MAFURIKO YA LOWASSA YAIPONZA TBC1, WAPEWA ADHABU NA TCRA KWA UBAGUZI HABARI ZA UKAWA



MAMLAKA ya mawasiliano nchini (TCRA) imekipa onyo kali kituo TBC1 kwa kosa la kubagua kusoma taarifa zinazohusiana na UKAWA.

Hukumu hiyo ilitolewa jana jijini Dar es Salaam na kamati ya maudhui ya utangazaji, katika ofisi za Mamlaka ya Mawasiliano na Kaimu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Walter Bugoya wakati wa mkutano na waandishi wa habari.


Bugoya alisema kamati hiyo imebaini TBC one imekiuka sheria ya utangazaji ya mwaka 2005 pamoja na sheria ya uchaguzi ya mwaka 2015 kwa kufanya upendeleo wa vyama katika taarifa zake kwenye kipindi.

Alidai katika kipindi cha Jambo Tanzania kilichorushwa tarehe 15 mwezi huu majira ya saa 12 asubuhi hadi saa tatu, katika kipingele cha uchambuzi wa magazeti mtangazaji wa kipindi hicho alikuwa anayasoma magazeti huku akiruka kusoma habari kuu husika.

Alisema Mtangazaji huyo alipokuwa anachambua gazeti la Majira na Nipashe alidanganya umma jambo ambalo amedai ni kosa.

Bugoya alitaja makosa hayo kuwa ni wakati mtangazaji huyo alipokuwa anasoma Gazati la Majira ukurasa wake wa mbele alisema habari kubwa ni “CCM yazidi kuwaumbua wanaomfuata lowassa” wakati habari kubwa ilikuwa inasomeka hapo ni ile inayosema “Mbeya kwafurika”, huku picha ya gazeti hilo likionyesha picha ya umati watu pamoja na mgombea wa Urais wa chadema Edward lowassa akihutubia.

Alisema mtangazaji huyo pia alifanya kosa lingine kama hilo pia wakati akisoma Gazeti la Nipashe ambapo alisema Habari iliyopewa uzito wa kipekee ni “Mbalawa atoa sheria ya mitandao” ambapo habari iliyopewa uzito ilikuwa ni ile “Mafuriko Mbeya” na sio aliyokuwa anaisoma yeye.

Alisema baada ya Kamati yake kubaini makosa hayo waliwasiliana na mkurugenzi wa TBC one Bwana Mshana.

Mkurugenzi huyo alitoa utetezi wake kwenye kamati hiyo akisema mtangazaji huyo hakufanya kosa kwakuwa alikuwa hajaridhika na taarifa zilizokuwa zimeandikwa kwenye magazeti hayo.

Sanjari na hayo Mshana alizidi kujitetea akidai kuwa hata mtangazaji huyo asingesoma habari ile lakini picha iliyokuwa inaonekana kwenye magazeti hayo tayari mtazamaji alikuwa ashajua kwahiyo amedai haikuwa na ulazima wa kusomwa.

Bugoya alisema baada ya kusikiliza upande wa TBC one ndio wakabaini kituo hicho kilikiuka sheria ya utangazaji ya Mwaka 2005 ambayo inavitaka vituo vyote vya utangazaji nchini kuripoti taarifa kwa kutokuwa na upendeleo wowote.

Alisema Kamati imefikia uamuzi wa kuipa onyo kali TBC one na endapo wataendelea basi Mamlaka hiyo haitasita kuwachukulia hatua kali zaidi.


ANGALIA HAPA CHINI TAARIFA ZAIDI

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527