MHESHIMIWA BERNARD MEMBE ATANGAZA NIA YA KUINGIA IKULU YA RAIS KIKWETE


WAZIRI wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, hivi punde ametangaza nia ya kuwania urais kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM) akiwa katika Viwanja vya CCM mkoani Lindi.

Kauli mbiu ya kiongozi huyo ni ‘Twende na Membe kwa Manadiliko ya Uhakika’.

Katika hotuba yake, Mhe. Membe amesema akipata fursa ya kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anataka watoto wa Tanzania wawe wenye afya na wapate elimu, wakina mama wasitembee umbali mrefu kufuata zahanati.

Pia amesema ataimarisha ulinzi na usalama maana nchi ipo kwenye matatizo ya kiusalama kama mauaji ya albino na madawa ya kulevya.

Katika sanaa na michezo, Waziri Membe amesema amedhamiria kuondoa dhana ya kwamba Tanzania ni kichwa cha mwenda wazimu katika michezo hivyo atahakikisha vyuo vingi vya michezo vinafunguliwa pamoja na kutoa fursa kwa wanamichezo kwenda nje ya nchi kupata uzoefu. Upande wa sanaa amesema atahakikisha wasanii wanapata haki zao za msingi kama hatimiliki na kulinda kazi zao.

Aidha Waziri Membe amesema akichaguliwa ataulinda na kuusimamia Muungano wa Tanganyika na Zanzibar maana ni wa kipekee duniani na ni tunu aliyotuachia baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere.

Membe ameongeza kuwa akichaguliwa ataziunganisha sekta binafsi na za umma ili kukuza uchumi na kuleta maendeleo sambamba na ajira.

Katika upande wa elimu, Mhe. Membe amesema ataweka mkazo katika Shule za Ufundi na Veta kwa kufufua vyuo vya ufundi maana ndiyo vinaongoza kwa kutoa ajira kwa vijana.

Waziri huyo pia ameeleza nia yake ya kupambana na rushwa ili kuleta utawala bora nchini.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post