WATAKIWA KUFANYA MIKUTANO YA ELIMU YA UKIMWI VIJIJINI,ACACIA YAPONGEZWA



Serikali wilayani Kahama mkoani Shinyanga kwa kushirikiana na mashirika mbalimbali imeshauriwa kuweka utaratibu wa kufanya mikutano mara kwa mara ili kutoa elimu  ya Ukimwi  hasa katika maeneo ya vijijini ambapo  jamii bado haijawa na uelewa wa kujikinga na maambukizi ya virusi vya Ukimwi.

Wakizungumza jana katika Tamasha la Siku ya Ukimwi Duniani, Baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Chapulwa Kata ya Mwendakulima wamesema  ipo haja ya serikali kufanya mikutano na wananchi hali itakayowasaidia wananchi kujitambua na kufahamu njia za kukabiliana na maambukizi ya VVU.

Baadhi ya wananchi hao, Diana Dotto na Leonald Paul  wameupongeza uongozi wa kampuni ya ACACIA kupitia mgodi wa Buzwagi kwa kubuni mbinu hiyo ambayo imesaidia vijiji vinavyozunguka mgodi huo kupata mwanga wa kutambua njia ya kujikinga na Ukimwi  kwa njia ya Hamasa za nyimbo na ujumbe wa viongozi mbalimbali.

Amesema elimu ya kupima ukimwi kwa hiari katika maeneo ya vijijini bado ni duni  ambapo hali hiyo inatokana na kutokuwepo kwa elimu inatotolewa na viongozi na kwamba viongozi wa vijiji na Kata wawe mstari wa mbele katika  kubuni hamasa ya kuelimisha jamii.

Afisa mahusiano wa Mgodi wa ACACIA- Buzwagi   David Kilala amesema  wameamua kufanya  mashindano ya kutafuta nyimbo bora yenye ujumbe mzuri wa kupinga maambukizi, na  unyanyapaa kwa watu wanaoishi na Ukimwi ili  kuishirikisha  jamii katika kupata ujumbe wa Ukimwi.

Amesema  pamoja na mambo mengine zoezi hilo la kushirikisha jamii pamoja na kufanya matamasha ni endelevu kwa kata ya Mwendakulima  ambapo watatumia nafasi hiyo kuielimisha jamii mbinu za kupunguza maambukizi ya Ukimwi pamoja na shughuli zingine za maendeleo.

Siku ya Ukimwi Duniani huadhimishwa Desemba Mosi kila mwaka na maadhimisho ya siku hiyo katika Mkoa wa Shinyanga yafanyika katika Kata ya Lunguya halmashauri ya Msalala wilayani Kahama.


Na Ndalike Sonda-Kahama

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527