JAMAA AHUKUMIWA KUNYONGWA KWA KOSA LA KUUA MAMA MKWE WAKE KWA MKUKI HUKO GEITA



Mahakama kuu inayoendelea mjini Geita mkoani Geita imemhukumu adhabu ya kunyongwa hadi kufa  Mathias Tangawizi(46) mkazi wa kijiji cha Ibondo katika kata ya Katoro wilayani Geita baada ya kupatikana na kosa la kumuua mama mkwe wake aitwaye Sofia Kamuli (51)mwaka 2008.

Akisoma hukumu hiyo jaji wa mahakama kuu Richard Malima amesema kuwa mtuhumiwa alitenda kosa hilo  tarehe 24 mei 2008 ambapo inadaiwa kuwa mama mkwe alikuwa anamtaka mtoto wake aachane na mme wake kwani alikuwa na uwezo mdogo wa kimaisha na baada ya kupata taarifa hizo mtuhumiwa ndipo alipotenda kosa hilo dhidi ya mama mkwe wake.

Awali mwanasheria  wa serikali Emiri Kiria aliiambia mahakama kuwa mnamo tarehe 24 mei 2008 huko katika kijiji  jirani cha Kaduda katika kata ya katoro majira ya saa 3.30 asubuhi mtuhumiwa alimfuata mama huyo na kumchoma mkuki sehemu za shingoni na tumboni hadi kufa.
Baada ya kufanya mauaji hayo  kwa kuchoma mkuki mama mkwe wake Sofia Kamuli (51)ambaye alikuwa mkulima,Mathias Tangawizi  alimtoa nje marehemu kwa kumvutia ndani na kufunga milango huku akitokomea kusikojulikana.

Ameongeza kuwa  baada ya siku mbili mtuhumiwa huyo alikamatwa kwani alikuwa amerudi katika kijij chake cha Ibondo ndipo jeshi la polisi lilimtia hatiani kwa kuhusika na mauaji hayo.

Aidha ushahidi uliotolewa na mashahidi saba kwa mfululizo umekuwa wa kuridhisha dhidi ya mtuhumiwa ambao haukuwa na mashaka yoyote hivyo na kuiomba mahakama itoe adhabu kali kwa mtuhumiwa huyo ili liwe fundisho kwa wengine wenye nia ya kutaka kutenda unyama huo.

Mara baada ya mahakama kusikiliza pande zote za mtuhumiwa na mlalamikaji ilijiridhisha kuwa mtuhumiwa alitenda kosa hilo kwa kudhamiria hivyo mahakama ikaamua kumtia hatiani kwa kunyongwa hadi kufa kwa mujibu wa kifungu cha 197 sura ya 16 cha mwaka 2002.

Kwa upande wa mtuhumiwa alijitetea kuwa apunguziwe adhabu kwa amekaa mahabusu kwa uUda mrefu hivyo angeweza kupunguziwa adhabu vilevile alijitetea kuwa mara baada ya kuingia mahabusu amekuwa akisumbuliwa na maradhi mbalimbali hivyo apunguziwe adhabu lakini Mahakama ilitupilia mbali maombi ya mtuhumiwa huyo.
 
 Na Valence Robert- Geita

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post