MARUFUKU KUVAA VIMINI BUNGE LA KATIBA

Wajumbe wanawake wa Bunge Maalumu la Katiba na wageni wa jinsi hiyo watakaovaa nguo fupi ‘vimini’ au nguo za kubana, hawataruhusiwa kuingia ndani ya Ukumbi wa Bunge.
Hayo yamo katika mapendekezo ya rasimu ya kanuni za uendeshaji wa Bunge hilo, zilizowasilishwa katika semina mahsusi ya kupokea rasimu hizo, iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa Kamati Maalumu, Profesa Costa Mahalu.

Kanuni ya 82 (9) ya mapendekezo hayo imeainisha vazi rasmi linaloruhusiwa kuwa ni vazi lolote la heshima ambalo siyo la kubana mwili, lisiloonyesha maungo.

Pia imeainisha mavazi yanayoruhusiwa kwa wanawake kuwa ni pamoja na gauni la kitenge au blauzi inayovaliwa na kitenge au sketi ya rangi yoyote, suti ya kike, vazi linalovaliwa wakati wa eda na kilemba cha kadri au mtandio.

Kwa upande wa wanaume, mavazi rasmi ni suti ya Kiafrika au safari ya mikono mirefu au mifupi yenye ukosi au shingo ya mviringo na fulana.

Kulingana na kanuni hiyo, upande wa wanaume, pia imeainisha vazi rasmi kwa jinsia hiyo kuwa ni suti ya Kimagharibi, shati na tai, suruali ya aina yoyote isipokuwa suruali aina ya ‘jeans’.

Sehemu ya 6 ya kanuni hiyo, imeweka wazi kuwa mjumbe yeyote wa Bunge Maalumu, anaweza kutoa taarifa kwenye Bunge au kwenye kamati iwapo mjumbe mwingine ataingia akiwa amevaa vazi linalovunja au kukiuka masharti ya kanuni.

“Mwenyekiti wa Bunge Maalum au mwenyekiti wa kamati maalumu atakaporidhika kuwa mjumbe huyo aliyetolewa taarifa hajavaa vazi rasmi, atamwamuru atoke nje ya ukumbi wa mikutano wa kamati,” inaseme sehemu ya kanuni hizo.

Kwa mujibu wa kanuni hiyo, mjumbe aliyeamriwa kutoka nje ya ukumbi, hataruhusiwa kuingia tena hadi pale atakapokwa amevaa mavazi rasmi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments