MKUU WA MKOA WA SHINYANGA ALLY NASSORO RUFUNGA AWATAKA WACHIMBAJI HARAMU WA MADINI KATIKA MGODI WA MWADUI KUACHANA NA UCHIMBAJI HUO

Shimo lililochimbwa na wachimbaji haramu ndani ya Mgodi wa Almasi wa Mwadui, wachimbaji hao huchimba usiku wa manane kwa kutumia vifaa visivyo vya kitaalamu hivyo kuhatarisha maisha yao

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Ally Nassoro Rufunga akishuhudia shimo hilo alipotembelea kuona shughuli za wachimbaji haramu katika mgodi wa Mwadui wilaya ya Kishapu jana akiwa ameambatana na viongozi mbalimbali akiwemo mkuu wa wilaya ya Kishapu Wilson Nkhambaku

Wachimbaji haramu wakiwa mbali baada ya kuona msafara wa Mhe. Mkuu wa Mkoa ukielekea eneo hilo, walitimua mbio lakini walirudi baada ya kuitwa sana na kuhakikishiwa usalama ndipo walipokubali kuongea na Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga


Mkuu wa Mkoa akizungumza na wabeshi hao(wachimbaji Haramu) alipowakuta eneo hilo hatari wakiendelea na shughuli hiyo.picha zote na Magdalena Nkulu afisa habari ofisi ya mkuu wa mkoa wa Shinyanga




Kufuatia kukithiri kwa vitendo vya uchimbaji haramu wa madini katika mgodi wa almasi wa Mwadui,Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Ally Nassoro Rufunga amelaani na kukemea tabia ya baadhi ya wananchi kuvamia maeneo ya migodi kwa lengo la kuiba mchanga wa madini kwa kuwa ni kinyume cha sheria na kuahidi kuwasaidia wachimbaji hao haramu maarufu kwa jina la Wabeshi  katika kupata ajira mbadala.


Mkuu huyo wa mkoa ametoa tamko hilo jana alipotembelea mgodi wa almasi Mwadui katika wilaya ya Kishapu na kujionea hali ya uchimbaji haramu unavyofanyika katika mgodi huo pamoja na kuzungumza na wachimbaji hao haramu.


Amesema kitendo hicho ni hatari kwa maisha ya wananchi hao na kuongeza kuwa serikali mkoani Shinyanga itawasaidia wachimbaji hao kutafuta shughuli mbadala ya kufanya na kuwataka waachane na shughuli hiyo mara moja.


Rufunga amesema serikali itahahakisha wanapata ajira halali kupitia viwanda vilivyopo na vinavyoendelea kujengwa mkoani Shinyanga, kuwakopesha mitaji kwa mfuko wa maendeleo ya vijana wa asilimia 5, pamoja na kufanya taratibu za kuwapatia maeneo madogo ili wachimbe kihalali endapo wataachana na uchimbaji haramu wa madini.


Amesema aina hiyo ya uchimbaji huo ni kuwaibia wawekezaji na kuwakwamisha kulipa mapato kwa serikali,kwani nchi inapata kodi kutoka kwa wawekezaji waliopata leseni halali ya uchimbaji,kodi ambayo inawanufaisha wananchi wenyewe katika shughuli za maendeleo.


Naye Meneja Mkuu wa Mgodi wa Mwadui Arlen Loehmer ameishukuru serikali kwa ushirikiano inaouonesha kwa mgodi huo ikiwa ni pamoja na kusaidiana  katika kujua na kutatua changamoto mbalimbali na kwamba  mahusiano hayo mazuri yanaimarisha juhudi za uwekezaji.


Kwa upande wao wachimbaji hao wamekiri mbele ya Mkuu wa Mkoa kuwa,ni kweli wanafahamu kazi hiyo siyo halali na kuahidi kuachana nayo kama watasaidiwa shughuli mbadala kwani wanafanya hivyo kujitafutia riziki kutokana na hali ngumu ya maisha na masharti ya mikopo kuwa ni magumu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post