Na Sheila Ahmadi, Ruangwa
Naibu Waziri wa Madini, Steven Kiruswa, amewataka wananchi wa Mkoa wa Lindi kutumia fursa zinazotokana na sekta ya madini kwa kufanya uchimbaji, biashara na kutoa huduma mbalimbali zinazohitajika katika maeneo ya migodi.
Kiruswa amesema sekta ya madini haipaswi kuonekana kuwa ni fursa kwa wachimbaji pekee, bali wananchi wanaweza kunufaika kupitia shughuli za biashara na huduma zinazozunguka shughuli za uchimbaji.
Amesema hayo wakati akizungumza katika hafla ya kufunga Maonesho ya Madini Ruangwa, Lindi Mining Expo 2026, ambapo amewataka wananchi wa Lindi kuongeza ushiriki wao katika sekta hiyo ili kunufaika na fursa zinazopatikana.
“Wananchi wa Lindi wanapaswa kuamka na kutumia fursa zilizopo katika sekta ya madini. Siyo lazima kila mtu awe mchimbaji; kuna fursa za biashara na utoaji wa huduma mbalimbali zinazohitajika katika maeneo ya migodi,” amesema Kiruswa.
maonesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu kwa wadau kujifunza, kutafuta masoko na kutambua fursa mpya za kiuchumi, huku akiwapongeza washiriki kwa juhudi zao za kutoa huduma na elimu kwa wananchi.
zaidi ya watu 500 wamepatiwa mafunzo mbalimbali katika maonesho hayo, yaliyolenga kuongeza uelewa na kuwajengea uwezo wachimbaji, wafanyabiashara na wadau wengine kuhusu fursa zilizopo katika sekta ya madini.
Aidha, amezitaka taasisi za fedha, ikiwemo benki, kuendelea kushirikiana na wachimbaji na wafanyabiashara kwa kuwawezesha kupata mikopo itakayosaidia kukuza shughuli zao.
Vilevile amewataka wachimbaji kutumia elimu waliyoipata kuhusu sheria, kanuni na mbinu za kisasa za uchimbaji ili kuongeza tija, usalama na thamani katika shughuli zao.



Social Plugin