Na mwandishi wetu
Msemaji wa Jeshi la Polisi, Naibu Kamishna wa Polisi DCP David Misime amesisitiza umuhimu wa Wanafamilia na jamii kwa ujumla kuishi kwa upendo kwa kuzingatia unyenyekevu pamoja na kufuata mafundisho ya Mwenyenzi Mungu ili kuwa na mwisho mwema hapa duniani.
DCP Misime ameyasema hayo leo Jumanne Juni 23, 2026 kwenye Viwanja vya FFU Mkoani Tabora wakati wa ibada ya kumuaga aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora Ex SACP Richard Abwao aliyefariki dunia mwishoni mwa Wiki iliyopita akipatiwa matibabu Jijini Dar Es Salaam, akibainisha kwamba kifo cha Afande Abwao kiwakumbushe wananchi wote umuhimu wa kuishi kwa upendo na unyenyekevu hapa duniani.
"Twendeni tukapatanishe nyumbani, na Nyumba zetu za ibada pamoja na Viongozi wa dini na wananchi kwa ujumla kwa yanayoonekana duniani sasa hivi kifo hiki kitukumbushe kurudi kwenye familia zetu, tutengeneze watu wanaothamini upendo, wanaothamini utu, wanaokua wanyenyekevu na waadilifu. Wazazi wenzangu twendeni kwenye familia tukatengeneze watu watakaokuwa na michango chanya kwenye jamii." Amesisitiza DCP Misime.
Katika hatua nyingine Msemaji huyo wa Polisi ametumia fursa hiyo pia kusisitiza jamii ya Watanzania kulinda watoto dhidi ya ukatili unaokatisha ndoto zao akibainisha pia kwamba kifo cha Abwao kiikumbushe jamii kuacha vita vya maneno kwani vita hivyo vinasambaratisha familia na Taifa kwa ujumla kwani chuki na uchonganishi haviwezi kuliacha Taifa likiwa na amani, utulivu na usalama.




Social Plugin