Na Sumai Salum- Kishapu
Wananchi wa Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga wameaswa kuchangamkia fursa ya upatikanaji wa miche ya miti bure inayotolewa na serikali kupitia Wakala wa Misitu Tanzania (TFS), kwa lengo la kuboresha mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Akizungumza katika zoezi la upandaji miti wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya Hiyo Mhe. Peter Masindi Machi 19,2026 Katika Kata ya Idukilo wilayani humo, Mhifadhi wa Misitu wa Wilaya ya Kishapu, Masatu Tumaini, amesema serikali imeondoa gharama za upatikanaji wa miche ya miti ili kuhakikisha kila mwananchi anapata nafasi ya kushiriki katika utunzaji wa mazingira bila kikwazo chochote.
Amebainisha kuwa jumla ya miche 4,000 imegawiwa kwa shule za msingi za Sanjo na Bulima pamoja na wananchi wa vijiji hivyo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha jamii inashiriki moja kwa moja katika uhifadhi wa mazingira.
Amesisitiza kuwa mawakala wanaendelea kuzalisha na kusambaza miche hiyo bure, huku akiwataka wananchi kuwa mabalozi kwa wengine ili kuhakikisha kila mmoja anapanda na kutunza miti.
Mwenyekiti wa Chama Cha ACT Wazalendo Wilayani humo Issa John, mbali na kupongeza juhudi za serikali kuhusu utunzaji mazingira kupitia upandaji miti, amewahimiza wananchi kusimamia na kulinda miti wanayoipanda, akieleza kuwa hilo ni jukumu la kila mtu na ni msingi wa maendeleo endelevu.
Viongozi mbalimbali wamepongeza juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuhamasisha utunzaji wa mazingira, pamoja na Mkuu wa Wilaya kwa kusimamia kwa karibu zoezi hilo.
Mratibu wa Mradi kutoka Shirika la Tcrs Mkoani Shinyanga Dkt. Oscar Rutenge, amesisitiza umuhimu wa umwagiliaji wa matone katika kuhifadhi miti hasa kipindi cha kiangazi, akiahidi kuendelea kutoa elimu kwa wananchi.
Kauli mbiu ya Siku ya Misitu Duniani inayosema Misitu ni uchumi, tuhifadhi kwa maendeleo ya taifa inaelezwa umuhimu wa misitu katika usalama wa chakula, lishe na maisha ya binadamu.
Tazama picha za matukio mbalimbali
Social Plugin