Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

NGORONGORO YANG'ARA KITAIFA NA KIMATAIFA KWA UTALII 2025


Na Woinde Shizza, Arusha

Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), Abdul-Razaq Badru, ametangaza kwa fahari kubwa kuwa Hifadhi ya Ngorongoro imetangazwa rasmi kuwa Kivutio Bora cha Utalii Barani Afrika kwa mwaka 2025, katika tuzo za kimataifa zilizofanyika Juni 28, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari katika mkutano uliofanyika  jijini Arusha, Kamishna Badru amesema ushindi huo ni matokeo ya juhudi za pamoja kati ya wadau mbalimbali wa utalii, wananchi, viongozi, wanafunzi wa vyuo na waandishi wa habari waliobeba ujumbe wa hifadhi hiyo kwa umahiri mkubwa.

“Ngorongoro tunatoa shukrani za dhati kwa kila mmoja aliyechagua kusimama nasi na kupiga kura. Ushindi huu si wa NCAA pekee bali wa Watanzania wote,” alisema Kamishna Badru huku akionesha tuzo mbili za ushindi huo

Kamishna Badru alieleza kuwa Ngorongoro si kivutio cha kitalii tu, bali ni hazina hai ya urithi wa kihistoria, maumbile ya kipekee na utamaduni wa asili. 

Alitaja maeneo yenye umuhimu mkubwa kama Nyayo za Laetoli zenye historia ya miaka milioni 3.6, Makumbusho ya Olduvai, Mlima Lomalasin (mlima wa tatu kwa urefu Tanzania) pamoja na uhamaji wa wanyama wa savana unaovutia kila mwaka.

Katika hotuba yake, aliwapongeza pia wageni wa kimataifa waliotembelea eneo hilo, wanafunzi wa vyuo waliounga mkono kampeni ya hifadhi, na waandishi wa habari waliowezesha ujumbe wa Ngorongoro kufika mbali.

Ngorongoro ni moja kati ya maeneo yaliyosajiliwa na UNESCO kama Urithi wa Dunia na Hifadhi ya Hai (Biosphere Reserve), jambo linaloiongezea hadhi ya kipekee katika uso wa dunia.


“Vivutio hivi kwa ujumla vinaiweka Ngorongoro juu na kuwa kivutio bora cha utalii Afrika kwa mwaka 2025,” alihitimisha Kamishna Badru.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com