Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

TANESCO YAZINDUA KAMPENI YA “LIPA DENI, LINDA MIUNDOMBINU, TUKUHUDUMIE”

Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa TANESCO, Bi. Irene Gowelle

Na Mwandishi wetu - Dar es salaam

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limewataka wateja wake wanaodaiwa kulipa madeni yao kwa hiari ili kusaidia Shirika hilo kujiendesha kwa ufanisi na kutoa huduma bora ya umeme kwa Watanzania.

Kupitia kampeni mpya iitwayo “Lipa Deni, Linda Miundombinu, Tukuhudumie”, TANESCO inalenga kuhamasisha ulipaji wa madeni kutoka kwa wateja wa malipo ya baada ya matumizi, sambamba na ukaguzi wa mita za LUKU kwa wateja wa malipo kabla. 

Kampeni hiyo imeanza kutekelezwa katika maeneo yote ya nchi.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa TANESCO, Bi. Irene Gowelle, amesema kampeni hiyo inalenga kuwahimiza wateja waliolimbikiza madeni kulipa kwa hiari kabla ya kuchukuliwa hatua za kisheria.

“Kupitia kampeni hii, wateja watakaolipa madeni yao kikamilifu watapewa motisha ikiwemo msamaha wa riba. Zoezi hili pia linahusisha ukaguzi wa mita za LUKU ili kuhakikisha zinafanya kazi vizuri na hazijachezewa,” amesema Gowelle.

Kauli mbiu ya kampeni hiyo ni “Huduma Endelevu Huanzia na Wewe”, ikilenga kuimarisha ushirikishwaji wa wananchi katika kulinda miundombinu ya umeme, ambayo ni mhimili muhimu wa maendeleo ya Taifa.

Aidha, Gowelle amesisitiza kuwa ulinzi wa miundombinu ya umeme si jukumu la TANESCO pekee, bali ni wajibu wa kila mwananchi.

“Tunahamasisha ulinzi shirikishi ili wananchi watoe taarifa kwa vyombo husika kuhusu vitendo vya wizi au uharibifu wa miundombinu ya umeme. Hili litasaidia kupunguza athari za kukatika kwa umeme na kulinda mali za umma,” ameongeza.

TANESCO imewahimiza wananchi wote kushirikiana na Shirika hilo kwa kutoa taarifa kuhusu wizi wa umeme na uharibifu wa miundombinu, ili kuzuia hasara na kuhakikisha huduma ya umeme inaendelea kupatikana kwa ufanisi nchini kote.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com