MASHIRIKA YASIYO YA KISERIKALI YAHIMIZWA KUBORESHA UTOAJI HUDUMA KWA JAMII

 

NA WMJJWM - Dodoma

Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yamehimizwa kuendelea kuboresha utoaji wa huduma zao katika Jamii licha ya uwepo changamoto mbalimbali.

Wito huo umetolewa na Afisa Ufuatiliaji na tathmini kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Modesta Komba Juni 07, 2024,  akizungumza kwa niaba ya Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, baada ya ziara ya kukagua Shirika la Action for Community Care linaloshughulikia Makundi yanayoishi katika mazingira magumu katika kuboresha maisha yao kielimu, afya, ulinzi na usalama jijini Dodoma.

"Tunawapongeza kwa kuendelea kusaidia jamii kwa kuboresha maisha ya Makundi mbalimbali yenye uhitaji pia nawaomba muendelee kuboresha utoaji wa huduma zenu kwa jamii, hususani kufanya usajili wa kituo cha kulelea watoto mchana, boresheni kituo hicho kwa usalama wa afya ya watoto na kuendelea kutatua changamoto wanazopitia wanufaika wa miradi yenu" amesema Modesta 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shirika hilo Pendo Maiseli ameahidi kuendelea kuboresha maeneo yote yaliyoelekezwa pamoja na kuendelea kutatua changamoto mbalimbali katika kusaidia jamii, huku akielezea changamoto za kifedha kuwa ni moja ya changamoto wanazokumbana nazo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Mtaa wa Hamvu Kata ya Chang'ombe ambapo Shirika linasimamia vikundi vya ujasiriamali Khalidi Majid amelishukuru Shirika hilo kwa kuwanufaisha na msaada wa mizinga ya nyuki na mitaji kwa vikundi mbalimbali katika Kata hiyo iliyowasaidia kuanzisha shughuli za ulinaji wa asali.

"Uwezeshaji huu umewasaidia wananchi kuongeza kipato chao kwa kuwa na shughuli ya kiuchumi kupitia Vikundi vya wajasiriamali na umebadilisha maisha ya wengi, tuendelee kushirikiana kuwainua wananchi kiuchumi" ameongeza Majid

Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, imeendelea kufanya ufuatiliaji wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali inayotekelezwa na Mashirika hayo na changamoto zilizopo.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post