WIZARA YA MALIASILI NA UTALII KUSHIRIKIANA NA WIZARA YA MAENDELEO YA JAMII KUWEZESHA WANAWAKE KIUCHUMI


Na John I. Bera 

Wizara ya Maliasili na  Utalii   kwa kushirikiana na  Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu zimepanga  kushirikiana kimkakati ili kuwawezesha wanawake  kiuchumi  kupitia fursa mbalimbali  zinazopatika kwenye sekta ya Maliasili na Utalii.


Kauli hiyo imetolewa leo Machi 9, 2024  na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima (Mb) alipotembelea Banda la  Maliasili na Utalii kwenye  Maonesho ya Wiki ya Wanawake Duniani yanayofanyika kwenye Viwanja vya Mashujaa Jijini Dodoma


Mhe. Gwajima amesema Wizara yake ni Wizara mtambuka ambayo utendaji  kazi wake unategemea Wizara zingine ikiwemo Wizara ya Maliasili na Utalii  


"Natambua kuwa ninyi ni wadau wetu muhimu  kwa sababu sisi Wizara ya Maendeleo ya Jamii hatuwezi kuendelea pekee yetu pasipo sekta nyingine  ikiwemo sekta ya Maliasili na Utalii", amesema Mhe. Gwajima.

Mhe. Gwajima amesisitiza kuwa   ili kuwafikia wanawake katika maeneo  mbalimbali nchini wizara za kisekta haziwezi kuachwa pembeni ikiwemo Wizara ya Maliasili na Utalii.


Aidha, Waziri Gwajima ameipongeza  Wizara ya Maliasili kwa kushiriki kwenye Maonesho hayo huku akisisitiza kuwa anaamini ya kuwa Wizara hiyo itaendelea kushirikiana na Wizara yake kuhakikisha kuwa  Wanawake wanajihusisha na shughuli za utalii nchini.


Akizungumza mbele ya Waziri Gwajima, Afisa Wanyamapori Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Africo Mattogoro amesema wao kama Wanawake kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii wanayo  ari ya kufanya kazi ya uhifadhi na usimamizi endelevu wa Rasilimali za Wanyamapori na maeneo oevu kwa ajili ya kuunga mkono agenda ya Rais Mhe. Dkt.  Samia Suluhu Hassan kupitia Filamu yake ya “The Tanzania Royal Tour’’


Ameongeza kuwa  wao kama Wanawake ambao  ni  Wahifadfhi kutoka  Wizara hiyo wanaendelea na   jitihada mbalimbali za  kuelimisha jamii kuhusu suala zima la uhifadhi  hususani kwa  wakinamama ambao wamekuwa wakiingia kwenye maeneo ya Hifadhi na kuendesha  shughuli za kibinadamu bila kujua ya kuwa wanaharibu mazingira na uhifadhi kwa ujumla


 Amesema  Wizara kwa kushirikiana na Taasisi zake imekuwa  ikitumia njia mbalimbali za kuwezesha Wanawake ikiwemo kutumia Vikundi mbalimbali kama COCOBA na njia nyinginezo kwa  lengo la kuinua uchumi wa wanawake wa Kitanzania. Jitihada hizo zinafanikiwa kwa kupitia taasisi za uhifadhi zilizopo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii  kama vile TANAPA, TAWA, TFS, NCAA na kwa kushirikiana na wadau wa mbalimbali wa Uhifadhi kwa kuwawezesha wananchi kupitia vikundi  kwa kuanzisha na kuwawezwsha shughuli mbadala rafiki na mazingira mfano ufugaji nyuki.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post