SILINDE AWATAKA WATANZANIA KUONDOA SHAKA UPATIKANAJI WA SUKARI NCHINI

Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. David Silinde (Mb) amewataka Wananchi kuondoa shaka juu ya upatikanaji wa sukari kwani Serikali kwa kutambua changamoto hiyo tayari imetoa vibali vya uingizwaji sukari ambapo meli zimeshatia nanga Bandarini zenye mzigo wa tani 100000 za sukari huku jitihada za uzalishaji sukari kwa viwanda vingine zikiendelea.


Mhe. Silinde ametoa wito huo wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Bishara, Kilimo na Mifugo ilipotembelea Viwanda vya Sukari vya Mbigiri na Mtibwa vilivyo katika Mkoa wa Morogoro leo Januari 29, 2024 ili kujionea hali ya uzalishaji wa sukari katika viwanda hivyo. 


Awali akitoa taarifa kwa Kamati hiyo, Mkurugenzi wa Kiwanda cha Sukari cha Mbigiri, Selestine Some amesema kuwa kiwanda hicho kina uwezo wa kuzalisha tani 50,000 kwa mwaka huku asilimia 50 ni kwaajili ya matumizi ya nyumbani.


Katika kuongeza tija ya uzalishaji, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Bishara, Kilimo na Mifugo imekitaka kiwanda hicho kuendelea kusimamia uzalishaji na kuhakikisha ufungaji wa mitambo mipya ya uchakataji sukari ya viwandani unakamilika ili kuchochea uzalishaji mkubwa wa sukari na kupunguza tatizo la upungufu wa sukari nchini.


Pamoja na mambo mengine Kamati hiyo pia imeshuhudia athari za mvua kubwa iliyorekodiwa kuwa 729.49mm ambayo ni kiwango kikubwa na mara tatu zaidi kuliko mvua iliyonyesha miaka mitatu iliyopita kwa wastani wa 288mm zilizonyesha maeneo mbalimbali mkoani Morogoro na kuleta athari mbalimbali hasa za uzalishaji katika sekta ya kilimo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post