WILAYA YA KONGWA YAMTUNUKU RAIS SAMIA TUZO YA URITHI WA HISTORIA

 

Na Dotto Kwilasa,Dodoma

Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa mkoani hapa imemtunuku Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan tuzo ya heshima ya  kutunza na kulinda urithi wa historia ya wapigania uhuru wa Nchi za kusini mwa Afrika na kuchochea utalii nchini.

Nchi hizo ni pamoja na  Zimbabwe, Angola, Afrika Kusini, Namibia na Msumbiji ambazo Ziliweka kambi wilayani hapo wakati wa harakati za kutafuta uhuru wa nchi za Afrika ambapo  Watanzania Walishiriki katika kutoa msaada kwa nchi hizo. 

Hayo yalielezwa mwishoni mwa wiki wakati wa  mbio za marathon zilizopewa jina la  Kongwa African Liberation Marathon zilizobeba kauli mbiu ‘Kongwa mbeleko ya ukombozi wa Afrika’.

Akikabidhi tuzo hiyo kwa mgeni rasmi ambaye alikuwa mkuu wa wilaya ya Chemba Gerald Mongela ,Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Remidius Mwema amesema lengo ni kuunga mkono juhudi za Rais Samia katika kutangaza vivutio vya utalii na kulinda urithi wa taifa.

Awali akizungumza wakati wa mkutano Mongela amesema wilaya ya Kongwa ni miongoni mwa maeneo yenye mandhari nzuri inayofaa kwa uwekezaji utakaochochea utalii kutokana na kwamba eneo hilo ni kitovu cha Mkoa wa Dodoma. 

“Tuendelee kuitunza historia ya Tanzania kwani moja ya ajenda ya Rais Samia amekuwa akisisitiza  kuhakikisha jamii inatambua historia ya nchi yao ili kuwa katika nafasi nzuri ya kulinda na kuiendeleza, ndani ya historia hii kuna mila, desturi, lugha, urithi, uwajibikaji na uzalendo hii i fursa nzuri  kwa Watanzania  na Afrika kwa ujumla kutambua na kuendelea kujivunia mchango wa taifa la Tanzania katika ukombozi wa Afrika,” amesema

Aidha ameelekeza  mbio hizo kuwa endelevu kila mwaka na kwamba  maandalizi ya mwakani balozi za nchi zilizotumia eneo la Kongwa kupata mafunzo ya kijeshi  zihusishwe kwenye maandalizi ili kuwezesha washiriki kutoka kwenye mataifa yao na hivyo kuzifanya mbio za kongwa marathon kuwa za kimataifa.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Kongwa Remidius Mwema amesema Serikali kupitia Ofisi yake ina mpango wa kuboresha miundombinu katika maeneo  ya kihistoria wilayani hapo ili kuwa moja ya sehemu zitakazovutia watalii lengo ni kutangaza utalii na historia ya ukombozi wa nchi za kusini mwa afrika.

Mwema ameeleza kuwa hatua hiyo itasaidia kuenzi maeneo hayo ikiwa ni pamoja na kutambua mchango wa Tanzania katika ukombozi wa nchi za kusini mwa Afika na kwamba maeneo yote yaliyotumiwa na wapigania Uhuru yatabaki kuwa kumbukumbu ya kipekee. 

Mkuu huyo wa wilaya ya Kongwa amezitaja nchi hizo ambazo viongozi wake waliweka kambi wilayani hapo kuwa ni takribani nchi tano ambazo ni Afrika Kusini, Namibia, Zimbabwe, Msumbiji na Angola. 

"Ni muhimu Sehemu ya fedha zitazopatikana kwenye mbio hizo kusaidia kuboresha maeneo ya kihistoria yanayo patikana wilayani hapa hususani  maswala ya  kielimu hasa ukarabati wa madarasa yaliyotumiwa na madawati, " amesema

Naye,Msimamizi na mratibu wa Kituo cha Urithi wa Ukombozi wa Afrika Boniface Kadili amesema kuwa Kongwa inakwenda kuingizwa kuwa kituo cha urithi wa taifa na baadaye  kwenye urithi wa dunia kwani ina vigezo vyote.

Amesema hatua hiyo ni muendelezo wa program ya urithi wa ukombozi wa Bara la Afrika wenye lengo la kutambua na kuhifadhi kumbukumbu za harakati za kutafuta uhuru wa nchi za Afrika ambapo nchi ya Tanzania ilishiriki katika kutoa msaada kwa nchi hizo. 

Amesema katika mwaka wa fedha 2023/2024 Wizara kupitia kituo cha urithi imetenga fedha maalum kwa ajili ya kufanya ukarabati wa mahandaki yaliyotumiwa na viongozi  wa nchi za kusini mwa Afrika  ikiwemo handaki la Kongwa ambalo lilitumiwa na hayati Samora Machel akiwa kongwa kwa ajili ya kujihami na hatari.

"Nitumie fursa hii kuelekeza kuwa maadhimisho ya  siku ya Afrika ambayo hufanyika Mei 25, kila mwaka,  yafanyike hapa Kongwa  kitaifa ili kuendelea kuitangaza eneo hili na  kuendelea kutoa elimu  kwa umma kuhusu utaliii uliopo Kongwa, " amesema

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa, White Zuberi ametumia nafasi hiyo kueleza  kuwa tangu mwaka 2010 wamekuwa wakipambana ili kufanya Kongwa ipate hadhi inayostahili.

Amesema  mara kaadha amekuwa akipokea ugeni kutoka nchi mbalimbali za Afrika ambao wanakuja kwa lengo la kuona makaburi ya mashujaa wao wa ukombozi lakini bado hawaoni umuhimu wa kuyahifadhi na kuyatunza kwa ajili ya kuyaenzi kwa manufaa ya vizazi vijavyo. 

“Mwaka 1995 kikosi cha Jeshi kiliondolewa Kongwa baada ya wapiganaji kuondoka  lakini tunashukuru sasa Rais Samia Suluhu Hassan amerudisha kambi ya Jeshi kwenye eneo la kihistoria,” amesemamafunzo

Wilaya ya Kongwa ni moja ya maeneo yaliyotumiwa na wapigania uhuru wa Bara la Afrika ambapo yanapatikana makaburi ya wapigania uhuru waliopoteza maisha wakati wa vita vya ukombozi pamoja na handaki la kijeshi lililotumiwa na Rais wa Msumbiji Samora Machel kwa ajili ya kujificha .



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post