WATOTO WA MWALIMU WAUAWA KWA KUKATWA MAPANGA...WATUHUMIWA WADAKWA MAPENZI YATAJWA


Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Katavi Kaster Ngonyani


Na Walter Mguluchuma - Malunde 1 blog Katavi .

Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi linawashikilia watu wawili wakazi wa Kitongoji cha Kabatini Kijiji cha Mpembe Wilaya ya Tanganyika Mkoa wa Katavi kwa tuhuma za kuwaua kikatili watoto wawili kwa kuwakata kata kwa mapanga wakiwa ndani ya nyumba ya mama yao.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Katavi Kaster Ngonyani amewataja watuhumiwa hao wawili wanaoshikiliwa na jeshi la polisi kwa tuhuma za mauaji hayo ya kikatili kuwa ni Dotto Mathias Machia(37) na Kija Maige(25) wote wakazi wa Kitongoji cha Kabatini Wilaya ya Tanganyika .

Tukio hilo la kusikitisha na la kikatili lilitokea Oktoba 3,2023  majira ya saa mbili asubuhi mara baada ya mama wa watoto hao kuondoka nyumbani na kwenda kazini  katika shule ya Msingi Kabatini anakofundisha .

Kamanda Ngonyani aliwataja watoto waliouawa kuwa ni Mariamu Mtimvi (13) na Ester Zuberi Enock(2) uchunguzi wa awali unaonyesha chanzo cha mauaji ni mama wa mtoto Ester Enock kukataa kuwa na mahusiano ya kimapenzi na mmoja wa wathumiwa hao wawili.

Alieleza watuhumiwa hao wote wawili wanaendelea kushikiliwa na jeshi la Polisi kwa mahojiano zaidi na mara uchunguzi wa tukio hilo utakapokuwa umekamilika watuhumiwa hao watafikishwa Mahakamani ili wakajibu tuhuma zinazowakabili .

Mwenyekiti wa Kijiji hicho Abdalla Kashamili alisema alitapa taarifa majira ya mchana kuwa kwenye kitongoji chake cha Kabatini kuna tukio la mauaji ya watoto wawili limetokea la kuuawa kikatili kwa kukatwa katwa na mapanga wakiwa ndani ya nyumba waliokuwa wanaishi .

Hivyo alilazimika kutoka nyumbani kwake na kuelekea moja kwa moja hadi kwenye eneo la tukio na alipofika alikuta kwenye eneo hilo kuna umati mkubwa wa watu na aliingia ndani ya nyumba waliokuwa wakiishi marehemu hao na alikuta kuna miili ya marehemu wawili wa kike ikiwa chini na imekatwa katwa kwa mapanga .

Kashamili alisema kabla ya tukio hilo mama wa watoto hao aliamka asubuhi na kuanza kufanya usafi wa nyumba kama ilivyokawaida yake na ilipofika majira ya saa mbili alikwenda kazini kwake kwenye shule ya Msingi Kabatini na kumuacha marehemu Mariami akiwa na mtoto wake Ester ambaye alikuwa akimlea wakati akiwa kazini .

Ilipo fika majira ya saa nne asubuhi mwalimu alimwagiza mwanafunzi mmoja aende nyumbani kwake akachukue mtoto wake na ampeleke kwake shuleni lakini mwanafunzi huyo alipofika nyumbani kwa mwalimu alibisha hodi kwa muda mrefu bila kujibiwa hali iliyomfanya arudi kutoa taarifa na ndipo mwalimu aliamua kwenda mwenyewe na alipofika alikuta watoto hao wote wawili wakiwa wameuawa kikatili .

Misho

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments