NEMC YATOA ELIMU YA MATUMIZI SAHIHI YA ZEBAKI KWENYE MAONESHO YA TEKNOLOJIA YA MADINI GEITA


Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeendelea na utoaji wa elimu ya Matumizi sahihi ya Kemikali ya Zebaki bila kuathiri afya na mazingira katika Maonesho ya Sita ya Kitaifa ya Teknolojia ya Madini Mkoani Geita.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye Maonesho hayo wakati wa semina Mkurugenzi wa Tathimini ya Athari kwa Mazingira na Jamii (NEMC) Bi. Lilian Lukambuzi amesema wanashiriki katika maonesho hayo kwa ajili ya kutoa elimu kwa wachimbaji wadogo ambao hasa wamekuwa wakitumia Zebaki katika kuchenjua madini ya dhahabu.

"Hii imetokana na Mradi ambao tunausimamia unaolenga kuhifadhi mazingira na kudhibiti matumizi ya Zebaki, lengo letu waweze kuelewa na kuona shughuli ambazo wanazifanya katika uchenjuaji wa madini kwa kutumia zebaki zinawezaje kuathiri afya na mazingira". Amesema

Aidha, amesema elimu hiyo itawafanya waelewe ni namna gani wanaweza kutumia teknolojia mbadala ili waweze kuepuka madhara ya kiafya na mazingira katika matumizi ya Zebaki.

Kwa upande wake Mchimbaji mdogo wa dhahabu Mkoani Geita Bw. Alex Bawaziri ameipongeza NEMC kwa kuhakikisha inawapa elimu ya kutosha wachimbaji wadogo wa madini ya dhahabu katika matumizi ya zebaki kwenye uchenjuaji, hivyo watatumia elimu hiyo kuhakikisha wanajiepusha na matumizi yasiyosahihi ya Zebaki.

Nae mchimbaji mdogo wa dhahabu kutoka Mkoani Mwanza, Bi. Salome Kusekwa amesema mafunzo hayo yamewaelimisha hasa katika kujikinga na zebaki katika uchenjuaji wa madini ya dhahabu, hivyo atatumia elimu ambayo ameipata kwenda kuwaelimisha wachimbaji wenzake ambao wamekuwa hawana elimu ya matumizi sahihi ya zebaki.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post