DKT. RUTAYUGA AWATAKA WAKUU WA VYUO BINAFSI KUANZISHA PROGRAMU ZINAZOKIDHI MAHITAJI YA JAMII


Katibu Mtendaji wa NACTVET, Dkt. Adolf Rutayuga amewataka wakuu wa vyuo binafsi vya elimu na mafunzo ya ufundi stadi kuanzisha programu zinazokidhi mahitaji mbalimbali kwenye jamii.

Dkt. Rutayuga ameyasema hayo wakati akifungua awamu ya pili ya mafunzo kwa wamiliki na wakuu wa vyuo binafsi vya Mafunzo ya Ufundi Stadi kutoka Kanda ya Kusini na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini leo tarehe 12 Juni, 2023 mjini Morogoro.

‘’Lengo la mafunzo haya ni kuwajengea uwezo wakuu na wamiliki wa vyuo binafsi katika utoaji wa mafunzo ili kusaidia katika kukidhi mahitaji ya jamii na kutoa wataalam wenye ujuzi na umahiri’’alisema Dkt. Rutayuga

Aliongeza kuwa, nia ya Baraza ni kuvisaidia na kuvilea vyuo hivyo ili viweze kufikia malengo huku akiwasihi wamiliki/wakuu wa vyuo kufuata sheria, kanuni na taratibu za NACTVET ikiwa ni pamoja na kufanyia kazi mapungufu yaliyoainishwa vyuoni mwao ili kuendana na ubora unaohitajika.

Naye Bw. Nurudini Nhuva,(Mkurugenzi - Quality Development College) kwa niaba ya washiriki, amepongeza NACTVET kwa kuandaa mafunzo hayo yaliyowaleta pamoja na kusikiliza changamoto zao kwa maendeleo ya Elimu ya Ufundi Stadi nchini huku akiwashauri washiriki wengine kufuata Kanuni na taratibu zilizowekwa na NACTVET.

Miongoni mwa watumishi wa NACTVET walioshiriki katika kutoa mafunzo hayo ni pamoja na Dkt. Alex Nkondola, Mkurugenzi(Huduma za Taasisi),Dkt.Amani Makota, Mkurugenzi(Huduma za uendeshaji vyuo),Dkt. Hirst Ndisa(Meneja Kanda ya kusini) na Bw. Joha Fugutilo(Meneja Kanda ya Nyanda za Juu Kusini).

NACTVET ina jumla ya vyuo 1329 (VET- 805, TET- 465, FDC- 55) vya elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi inavyovisimamia nchini.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post