TAKUKURU SHINYANGA YABAINI DOSARI UGAWAJI WA PEMBEJEO ZA RUZUKU KWA WAKULIMA

Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga Donasian Kessy  akizungumza na waandishi wa habari 
Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga Donasian Kessy  akizungumza na waandishi wa habari 


Na Halima Khoya,Shinyanga.

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Shinyanga, imebaini vitendo vya rushwa katika zoezi la ugawaji wa pembejeo za ruzuku kwa wakulima wa Manispaa ya Kahama.

Akizungumza na vyombo vya habari leo mei 25 2023,Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga Donasian Kessy amesema kuwa serikali imekuwa ikiandaa miongozo mbalimbali ya utekelezaji wa shughuli za kilimo ambapo kati ya miongozo hiyo ni mwongozo wa utekelezaji wa mpango wa ruzuku mbolea msimu wa 2022/2023 ambapo serikali imelenga kupunguza makali ya bei ya mbolea, kuongeza uzalishaji, kuimarisha usalama wa chakula pamoja na upatikanaji wa malidhafi za viwandani.

Hata hivyo pamoja na kuwepo kwa Sheria, utaratibu na miongozo ya utoaji wa pembejeo za ruzuku,amesema wamebaini kuwepo kwa mianya ya rushwa katika hatua ya utekelezaji miongozo ambayo inaweza kutumika kuwanufaisha baadhi ya wadau.


"TAKUKURU Shinyanga ilifanya uchunguzi wa Mfumo wa utoaji wa pembejeo (mbolea) za ruzuku katika kata tatu za wilaya ya kahama(Zongomela,Busoka na Mwendakulima) na kubaini mapungufu katika Zoezi hilo", amesema Kessy


"Miradi mingine ya maendeleo iliyofuatiliwa ni pamoja na sekta ya elimu,afya,maji ujenzi na mikopo ya asilimia 10%,jumla ya miradi ya maendeleo 44 iliyotekelezwa yenye thamani ya Tsh.Bil 5.5 zilozoonekana na dosari ndogo ndogo.

TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga kushirikiana na wadau wa maendeleo imejipanga kuhakikisha elimu ya masuala ya rushwa inatolewa katika Taasisi za serikali,binafsi na wananchi ili kuongeza wigo wa mapambano dhidi ya rushwa.


Aidha kwa kipindi cha mwezi Aprili-Juni 2023 ambacho ni robo ya nne ya mwaka wa fedha 2022/2023,TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga imepanga kufanya vikao na wadau ambao ni watoa huduma ili kujadili kero zilizojadiliwa na wananchi katika kikao cha utambuzi wa kero ili kubaini/kuzuia rushwa katika utoaji wa huduma kwa jamii na utekelezaji wa miradi ya maendeleo.


" TAKUKURU inaendelea kutoa with kwa wananchi wote Mkoa wa Shinyanga kutoa ushirikiano kwa serikali, kuhakikisha miradi yote inayoendelea katika mkoa wetu inakamilika katika ubora,mkiona vitendo vyovyote vinavyoashiria ubadhilifu wa fedha za miradi hiyo toeni taarifa",ameongeza.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments