MAMBO INAYOZINGATIA EWURA KATIKA KUPANGA BEI


Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Bw. George Kabelwa akizungumza wakati wa kikao cha kukusanya maoni ya wananchi kuhusu maombi ya kurekebisha bei za huduma za Mamlaka ya Majisafi na usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA) kilichoandaliwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo Aprili 6,2023 jijini Dodoma.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,Rosemary Senyamule akizungumza wakati akifungua kikao cha kukusanya maoni ya wananchi kuhusu maombi ya kurekebisha bei za huduma za Mamlaka ya Majisafi na usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA) kilichoandaliwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo Aprili 6,2023 jijini Dodoma.
Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri,akizungumza wakati wa kikao cha kukusanya maoni ya wananchi kuhusu maombi ya kurekebisha bei za huduma za Mamlaka ya Majisafi na usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA) kilichoandaliwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo Aprili 6,2023 jijini Dodoma.
SEHEMU ya Washiriki wakifuatilia mada mbalimbali wakati wa kikao cha kukusanya maoni ya wananchi kuhusu maombi ya kurekebisha bei za huduma za Mamlaka ya Majisafi na usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA) kilichoandaliwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo Aprili 6,2023 jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa DUWASA, Mhandisi Aron Joseph,akitoa elimu kwa Wananchi wakati wa kikao cha kukusanya maoni ya wananchi kuhusu maombi ya kurekebisha bei za huduma za Mamlaka ya Majisafi na usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA) kilichoandaliwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo Aprili 6,2023 jijini Dodoma.


Alex Sonna,-DODOMA

MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imesema imekuwa ikizingatia masuala mbalimbali katika kutathmini maombi ya marekebisho ya bei za huduma husika ikiwa ni pamoja na gharama halisi ya uzalishaji, usambazaji na ufikishaji wa huduma husika kwa wateja.

Hayo yameelezwa leo Alhamisi Aprili 6,2023 na Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Bw. George Kabelwa,wakati akizungumza kwenye taftishi kuhusu maombi ya kurekebisha bei za huduma za maji za Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dodoma.

Bw. Kabelwa, ameyataja mambo mengine wanayozingatia ni pamoja na urejeshaji wa gharama za uwekezaji katika miundombinu na uzalishaji wa maji kwa kufanya uwekezaji mdogo wa miundombinu,mlinganisho wa gharama za uendeshaji na Mamlaka nyingine za maji hapa nchini,kulinda maslahi ya wateja pamoja na uendelevu wa huduma ya maji.

Aidha Bw. Kabelwa, amesema utaratibu wa kupitisha maombi ya kurekebisha bei za huduma una hatua kuu saba ambazo ni,kupokea maombi, Kupitia maombi na kuomba ufafanuzi pale inapohitajika, Mkutano wa hadhara (taftishi) ndani ya eneo ambalo mamlaka imeomba.

“Kupokea maoni ya maandishi,Kufanya uchambuzi wa kina na kuwasilisha mapendekezo kwenye Bodi ya EWURA,maamuzi ya bodi na hatua ya mwisho ni kutangaza maamuzi ya Bodi kwenye Gazeti la Serikali,”amesema Bw. Kabelwa,

Amesema katika Agizo hilo, EWURA itaainisha bayana misingi na hoja zilizopelekea maamuzi yake na masharti ambayo Mamlaka ya Maji Dodoma itatakiwa kuyazingatia katika utekelezaji wa agizo la bei.

Bw. Kabelwa, amesema sehemu kubwa ya masharti hayo yanalenga kuboresha huduma ya maji kwa wananchi ikiwa ni pamoja na kufikisha huduma ya maji katika maeneo ambayo kwa sasa hayana huduma hiyo.

Amesema kwa mujibu wa EWURA mtu yeyote asiyeridhika na uamuzi wa EWURA anayo haki ya kukata rufaa kwenye Baraza la Ushindani wa Haki Katika Biashara yaani (Fair Competition Tribunal), kwa kifupi FCT.

Bw. Kabelwa,amesema tangu kuanzishwa, EWURA imefanya mapitio na tathmini ya maombi ya kubadilisha bei za huduma za maji kwa Mamlaka za Maji za majiji na miji yote mikuu ya mikoa ambapo katika baadhi ya sehemu, mabadiliko hayo yamefanyika zaidi ya mara moja.

Aidha, EWURA imefanya mapitio na tathmini ya maombi ya kubadilisha bei katika baadhi ya miji ya Wilaya na Miji midogo. Ukiacha sekta ya maji, EWURA imefanya mapitio na tathmini ya maombi ya kubadilisha bei katika sekta ya gesi na nishati ya umeme na kufanya mabadiliko katika bei za huduma hizo.

“Katika maeneo yote hayo, na sekta nilizozitaja hapo juu, EWURA imekuwa na mfumo shirikishi wa kushirikisha wadau wote wakiwemo watumiaji wa huduma kama inavyofanyika leo kabla ya kupitisha maombi husika,”amesema Bw. Kabelwa,

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,Rosemary Senyamule amesema Serikali inatarajia utendaji mahiri, wenye kuzingatia uwazi wa EWURA ambao utakuwa chachu ya kuboresha utoaji wa huduma za majisafi katika mji wetu.

“Uwekezaji katika sekta hii utaongeza upatikanaji na ubora wa huduma hii na hivyo kuleta ufanisi endelevu na wenye kuzingatia uboreshaji wa mazingira kwa faida yetu na ya vizazi vijavyo,”amesema

Bi.Senyamule amewataka watoe maoni bila upendeleo wowote wakiwa na dhamira ya kuhakikisha kuwa kuna mizania kati ya watumiaji huduma za majisafi na usafi wa mazingira, Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dodoma na Taifa linafikia malengo yake

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments