POLISI WAFUKUA NYUMBA YA MWALIMU ALIYEDAIWA KUZIKA MKEWE NDANI

Polisi mkoani Geita wamelazimika kufukua ndani ya nyumba ya mwalimu Francis Elizeus wa shule ya msingi Lubanga baada ya ndugu wa mke wake kumtuhumu kuwa amemuua mke wake Jenifer Mashimo na kumfukia ndani hali iliyopelekea ndugu hao kumtishia maisha mwalimu huyo


Mke wa Mwalimu huyo inadaiwa alitoweka tangu Machi 2020

Kamanda wa Jeshi la polisi mkoa wa Geita Safia Jongo anasema walipata taarifa ya tukio hilo wakafuatilia kibali cha mahakama ili waweze kujiridhishaa juu ya uwepo wa mwili ndani ya nyumba ya wanandoa hao ambapo hata hivyo hawajaupata

“Tarehe 3, Kibali kilipatikana na zoezi la ufukuaji ulianza kwahiyo siku ya tarehe 3, tulifukua mashimo manne ndani ya nyumba ambapo wale ndugu walikuwa wanahisi hayo maeneo kwamba ndugu yao amefukiwa lakini mpaka ikafika usiku hatukuweza kufanikiwa"

Tarehe 5 zoezi lile pia likaendelea ambapo tulifukua kila eneo ambalo tulitilia mashaka kwamba linaweza likafukiwa mwili lakini hatima yake tulikiridhisha kabisa kila eneo ambalo linastahili kufukuliwa ndani ya ile nyumba na lile eneo ndani ya ule mji tulilifukua na hakuna mwili uliopatikana kwahiyo familia na wenyewe wamethibitisha kwamba hakuna mwili uliofukiwa” alisema Jongo.

Kamanda Jongo anasema kwa sababu za kiuchunguzi na usalama imewalazimu kumshikilia mwalimu huyo ili waweze kumuepusha na watu wanaomtishia Maisha.

“Kwahiyo sisi Kama Jeshi la Polisi, kwa sababu ndio kwanza tumepata hizi taarifa rasmi tutafanya utaratibu wa kuendelea kumtafuta jalada la uchunguzi hili sasa litaendelea kumtafuta kwa kuzitangaza picha zake kwenye magazeti kwenye vyombo mbalimbali vya habari ili kama bado yupo hai na yuko mahali Basi aweze kupatikana na hatua zaidi zichukuliwe"

"Mwalimu kwa sasa tunamshikilia kwa usalama wake kwa sababu Baba mzazi wa mwalimu alikuja pale nyumbani kufuatilia hili jambo na familia ilimtishia kwahiyo tunahofia usalama wake kwahiyo uchunguzi utakapokamilika wale ambao wanatishia usalama tutawachukulia hatua lakini huyu mwalimu bado tunamuhifadhi kwa ajili ya usalama wake”, alisema Jongo.

Kwa mujibu wa Kamanda Jongo anasema walimhoji mama wa Jenifer Mashimbo akakiri kwamba mwanae alikuwa ana tabia ya kuondoka nyumbani akigombana na mme wake na kurudi baada ya mwezi au miezi mitatu lakini imekuwa tofauti kwa kipindi hiki kwani tangu aondoke Machi 2020, hakuwahi kurudi hali iliyopelekea kuhisi mtoto wao ameuawa na mme wake na kuzikwa ndani ya nyumba.

Chanzo - EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments