HOSPITALI YA WILAYA YA MALINYI YAZINDUA HUDUMA YA KITENGO CHA MACHO

Hospitali ya wilaya ya Malinyi imezindua huduma ya kitengo cha macho ambapo sasa kimeanza kutoa huduma rasmi Machi 20 ,2023 na kuzinduliwa na Mkuu wa Wilaya ya Malinyi Sebastian Waryuba.

Kitengo hicho ambacho kimejengwa kwa thamani ya zaidi ya shilingi milioni 194 kutoka kwa wafadhili ambao Eye Care Foundation ambao mbali ya kujenga kituo hicho pia wametoa ufadhili wa kuwajengea uwezo wataalam wa macho katika hospitali ya wilaya ya Malinyi.

Kulingana na Mganga mkuu wa wilaya ya Malinyi Dkt. Aziz Keto kitengo cha macho kwa sasa kimewezeshwa vifaa vya kisasa ambavyo vitasaidia katika utoaji wa huduma za macho za kisasa kuanzia uchunguzi hadi upasuaji.

Upasuaji wa kwanza ukitarajiwa kufanyika Machi 21 mwaka huu kupitia wataalamu waliobobea katika sekta  ya macho.

Akizindua huduma katika kituo hicho mkuu wa wilaya ya Malinyi Sebastian Waryuba amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoka zaidi ya shilingi bilioni 2 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa hospitali hiyo sambamba na vifaa tiba Amesema kununuliwa kwa vijaa vya kisasa na elimu waliyopatiwa kuhusu utaalam zaidi wa macho iwe chachu ya kuwahudumia vema wagonjwa wote watakaofanyiwa huduma katika kituo hicho.

Mbali na kuwasisitiza watoa huduma katiuka kituo hicho kutoa huduma nzuri pia ametoa wito kwa jamii kuanza kula lishe bora ambayo itawasaidia kuondokana na matatizo ya macho.

“Ifikie ndugu zangu sasa tuanze kuhamasisha jamii kula lishe bora ambayo itasaidia kuondoa matatizo ya macho kwani sasa hivi watu wamekuwa na changamoto ya macho hii inaashiria kuacha kupata lishe bora kwa hito wataalamu wetu wasaidieni jamii kula lishe bora ambayo itawasaidia kutopata matatizo ya macho”alisema.

Awali Katibu Tawala wilaya ya Malinyi Bahati Joram aliwashukuru wafadhili waliojenga jingo hilo shirika la Eye Internationa Care ambao wameshirikiana na halmashauri katika kufikisha malengo ya kufunguliwa kwa huduma ya macho katika hospitali ya Wilaya ya Malinyi.

“Sio hawa wenzetu wa  Eye Care Foundation tunakaribisha na wengine waje wawekeze katika huduma za afya wilayani kwetu lengo letu ni ushirikiano mzuri baina ya serikali na mashirika pamoja na watu binafsi”alisema.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Malinyi  Absalom Gepson Mwasumbwe amesema kulingana na ripoti za kitengo cha macho katika hospitali ya wilayaya Malinyi kitengo cha macho kitapokea wagonjwa kutoka katika zahanati mbalimbali wilayani humo,vituo vya afya na hatimae wale ambao watagundulika na matatizo ya macho watapewa huduma zote katika kitengo hicho bila kufuata tena huduma katika wilaya zingine ama mikoa mingine.

Diwani wa kata ya Malinyi Mheshimiwa Said Tira ambae pia ni Mwenyekiti wa kamati za huduma za jamii amesema wananchi wa Malinyi hawajutii kutoa eneo kwa ajili ya ujenzi wa hospitali hiyo kwani sasa matunda yameanza kuonekana.

“Nimshukuru Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan ambae ametupatia vifaa vya kisasa kabisa katika hospitali hii ambapo vingine vimeshaanza kutumika katika hospitali hii hakika ni jambo la kujivunia sana”, alisema.

Baadhi ya wananchi walioshiriki uzinduzi huo wameishukuru serikali kuwezesha vifaa katika kitengo hicho na kusema sasa wataepukana na adha ya kufuata huduma ya macho nje ya wilaya ya Malinyi.“

Jambo hili la kupongezwa sana kwa maana sasa tutakuwa tumepata unafuu kupata huduma hapa hapa katika hospitali yetu “alisema Bi. Mariam Malambo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments