KAMATI YA SIASA YA CCM IMESELA YATAKA WATOTO WALE CHAKULA SHULENI


Diwani wa kata ya Imesela Seth Msangwa akizungumza katika maadhimisho ya ziara ya kamati ya siasa ya chama cha Mapinduzi (CCM) Imesela Wilaya ya Shinyanga.
Kamati ya siasa na uongozi wa shule wakiendelea na kikao cha kamati ya siasa Chama Cha Mapinduzi.

 Na Halima Khoya,Shinyanga.

Kamati ya Siasa ya Chama Cha Mapinduzi Kata ya Imesela  Halmashauri ya Shinyanga imeutaka uongozi wa Shule ya Msingi Mwamanyuda pamoja na kamati ya shule hiyo kuhakikisha watoto wanapata huduma ya chakula wakiwa shuleni ili kuongeza ufaulu kitaaluma.

Kamati hiyo imetoa agizo hilo katika kilele cha ziara ya Kamati ya chama Cha Mapinduzi iliyoanza Machi 7,2023 na kumalizika Machi 9 Mwaka huu kwa lengo la kutembelea taasisi mbalimbali na kukagua miradi iliyopo na kuangalia maendeleo na mikakati ya kukabiliana na changamoto mbalimbali.

Mwenyekiti wa CCM Kata ya Imesela,  Sebastiani Mwigulu  amesema ili kulijenga Taifa la baadae ni lazima kutoa elimu bora kwa watoto kwanzia shule ya msingi hadi sekondari sambamba na kupata lishe bora ili kuwa na  afya ya akili.

Hata hivyo Sebastian ameitaka kamati ya shule hiyo kuitisha kikao cha wazazi kwa ajili ya kuchangia fedha au nafaka kwa wanafunzi kupata chakula wakiwa shuleni hali itakayosaidia kuondokana na adha la utoro kwa wanafunzi.

Kwaaupande Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mwamanyuda, Charles Mmasa amesema awali waliitisha kikao na wazazi kwa ajili ya kuchangia chakula shuleni lakini wazazi hao waliikataa hoja hiyo kwa kudai hali ngumu ya maisha huku akiiomba kamati ya chama kutumia nafasi zao kuwahamasisha wazazi kutoa mchango wa chakula kwa watoto.

Jumanne Bundala na Christina Salehe ni wanafunzi katika shule ya Mwamanyuda ambao wameeleza ugumu wanaokabiliana nao kwa kusoma kuanzia asubuhi hadi jioni bila kupata chakula hali inayowafanya wasielewe masomo yao na kupelekea kufeli kwenye masomo yao.

"Tunapata changamoto nyingi sana tuwapo shuleni tunashinda njaa, hatuelewi masomo, tunawaombaa wazazi mjitokeze kuchangia chakula,na Serikali itusaidie kupata chakula ili tusome vizuri na kufaulu"amesema Bundala.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Imesela, Seth Msangwa amesema kuwa ili kutatua suala la chakula shuleni ni lazima kuruhusu sheria kuchukua mkondo wake kwa watakaoenda kinyume na makubaliano ya kuchangia chakula na kwamba wanawadumaza watoto kiakili kwa kukosa lishe bora.

"Suala la kupata chakula lipo ndani ya uwezo wetu,kile ambacho watoto walipaswa wale nyumbani ni sawaa sawa na kile ambacho watakula shuleni,iwe wakati wa njaa au hali ngumu basi kuchangia wazazi chakula inawezekana", amesema Msangwa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments