BIBI WA MIAKA 80 AUAWA AKIDHANIWA MWIZI... 'ALIKUWA ANAFUNUA PAZIA ANACHUNGULIA NDANI...."


Kamanda wa polisi mkoa Kigoma Kamishna Msaidizi wa polisi (ACP) Ramadhani Kingai (kushoto) akitoa taarifa kwa waandishi wa habari kuhusu kuuawa kwa bibi Kizee mmoja akidhaniwa kuwa ni  mwizi sambamba na matukio mbalimbali yaliyotokea mkoa Kigoma wiki hii. (Picha na Fadhili Abdallah)
Kamanda wa polisi mkoa Kigoma Kamishna Msaidizi wa polisi (ACP) Ramadhani Kingai (kushoto) akitoa taarifa kwa waandishi wa habari kuhusu matukio mbalimbali


Na Fadhili Abdallah,Kigoma


CHUBWA Kinyagala (80) Mkulima na mkazi wa kijiji Chilambo wilaya ya Kakonko mkoani Kigoma ameuawa kwa kupigwa na kitu kizito kichwani kwa kudhaniwa mwizi baada ya kuingia kwenye nyumba ya watu bila taarifa.

Kamanda wa polisi mkoa Kigoma, Ramadhani Kingai akitoa taarifa kwa waandishi wa habari mapema leo asubuhi alisema kuwa tukio hilo lilitokea mwanzoni mwa wiki hii majira ya saa tano usiku ambapo polisi imemtia mbaroni Rukia Buyoka (60) kwa tuhuma za kuhusika na mauaji hayo.

Kamanda Kingai alisema kuwa siku ya tukio marehemu Kinyagala alikuwa akirudi nyumbani kwake kutoka matembezi akiwa amelewa pombe ambapo akiwa kwenye hali ya ulevi aliingia kwenye nyumba ya Rukia Buyoka akidhani anaingia nyumbani kwake.

Alibainisha kuwa baada ya kufika kwenye nyumba hiyo marehemu alikuwa akifunua pazi na kuchungulia ndani ambapo Mtuhumiwa Buyoka alitoka na kumpiga marehemu na ubao mzito kichwani akidhani mwizi na marehemu alianguka papo hapo na kupoteza fahamu, Marehemu alifariki dunia akiwa njiani kukimbizwa hospitali ya wilaya Kakonko.

Pamoja na maelezo hayo Kamanda huyo wa polisi alisema kuwa mtuhumiwa baada ya kuona marehemu ameanguka hivyo kudhani ameua alitoka na kukimbia ambapo alitiwa mbaroni siku mbili baadaye.

“Mwili wa marehemu ulifanyiwa uchunguzi na polisi na baadaye kukabidhiwa kwa ndugu wa marehemu kwa ajili ya taratibu za mazishi ambapo upelelezi wa shauri hilo unaendelea ili mtuhumiwa aweze kufikishwa mahakamani,”Alisema Kamanda Kingai.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments