TANZANIA MWENYEJI MAADHIMISHO YA 16 YA SIKU YA BONDE LA MTO NILE

Katibu mkuu Wizara ya Maji Mhandisi Anthony Sanga (katikati) akiongea na Waandishi wa habari kuhusu maashimisho ya siku ya Bonde la mto Nile,kulia ni Mkurugenzi mtendaji wa NBI Sylvester Matemu na kushoto ni Mkurugenzi wa rasilimali maji kutoka wizara ya maji  Dkt. George Lugomela .

******

Na Mwandishi wetu-Malunde 1 Blog-DAR ES SALAAM.


MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho ya 16 ya siku ya Bonde la mto Nile yatakayofanyika 22, February,2022 Jijini Dar es Salaam .


Aidha jumla ya washiriki 1500 kutoka nchi mbalimbali duniani wakiwemo wajumbe wa baraza la Mawaziri wa nchi wanachama wa Bonde hilo,Mawaziri wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,wadau wa maendeleo ,Taasisi za Serikali na sekta binafsi watashiriki Mkutano huo.


Hayo yameelezwa leo Jijini Dar es Salaam na Katibu mkuu,Wizara ya Maji Mhandisi Anthony Sanga katika Mkutano wake na Waandishi wa habari kuhusu maashimisho hayo na kueleza kuwa hii itakuwa ni mara ya pili kwa Tanzania kuwa mwenyeji wa maadhimisho hayo baada ya kuandaa maadhimisho ya 11 mwaka 2017.


Amesema, Wizara ya Maji kwa kushirikiana na sekretarieti ya Bonde la mto Nile imeandaa maadhimisho hayo ili kutoa hamasa kwa watanzania kuenzi na kutunza vyanzo vya maji na uhifadhi wa mazingira kwa ujumla.


"Hii ni heshima kubwa kwetu,mara baada ya mkutano wa 29 wa baraza la Mawaziri wa nchi wanachama wa Bonde la mto Nile uliofanyika mjini Juba,Sudan Kusini tarehe 25,Novemba,2021 kuiteua Tanzania kuwa mwenyeji,"amefafanua


Licha ya hayo Dkt. Sanga ameeleza kuwa kauli mbiu ya maadhimisho hayo ni "Urithi wetu kwa amani na ustawi" ikilenga kuzikumbusha nchi wanachama wa Bonde la mto Nile kuona umuhimu wa ushirikiano katika usimamizi,uendelezaji na  matumizi ya maji ya Bonde hilo kwa ajili ya kudumisha amani na ustawi wa nchi wanachama.


Naye Mkurugenzi wa masuala ya umwagiliaji (NBI) Sylivester Matemu ameeleza kuwa ushirikiano wa mpito wa Bonde la mto Nile unajumuisha nchi 10 wanachama ikiwemo Tanzania yenyewe,Burundi, Ethiopia,Kenya na Jamhuri ya kidemokrasia ya watu wa Congo.


Amezitaja nchi nyingine kuwa ni Rwanda,Uganda, Sudan Kusini,Misri na Sudan na kufafanua kwamba ushirikiano huo ulianzishwa 22, February,1999 Jijini Dar es Salaam,Tanzania Kwa madhumuni ya ushirikiano katika usimamizi ,uendelezaji na uratibu matumizi sahihi ya rasilimali za maji ya Bonde hilo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments