RAIS SAMIA : VIJANA TAFUTENI KAZI SIYO AJIRA..NI AIBU KIJANA KUKAA BILA KAZI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akihutubia katika Maadhimisho ya kilele cha Matembezi ya Miaka 58 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar leo tarehe 07 Januari 2022 katika uwanja wa Makombeni Wilaya ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba
**

Rais Samia Suluhu Hassan amewataka Vijana nchini kujikita zaidi katika kutafuta fursa za kazi badala ya fursa za ajira. 

Rais ametoa wito huo leo Ijumaa, Januari 7, 2022 wakati wa kilele cha matembezi ya miaka 58 ya Mapinduzi ya Zanzibari huko wilaya ya mkoani Kusini Pemba.

Amesema ni lazima Vijana wakatambua kuwa ajira ambazo zimekuwa zikitangazwa hazitoshi, hivyo ni lazima wakajielekeza katika kufanya kazi ambazo zitawaingizia kipato chao cha kila siku.

“Natambua changamoto kadhaa zinazowakabili na changamoto ya kwanza inayowakabili ni ajira. Kwahiyo, hili tunalitambua na tunatambua kwamba ukosefu wa ajira ni changamoto ya Dunia nzima na kila mabadiliko Duniani yanapotokea tatizo hili linazidi kubwa zaidi.

“Katika kipindi cha miezi 9 ya serikali ya awamu ya sita, serikali imetoa ajira zipatazo 14,000 na serikali itaendelea kuangalia fursa mbalimbali zitakazotoa ajira kwa vijana wetu. Nawaomba vijana mkaangalie fursa za kazi, fursa za kazi zipo nyingi. Ni aibu vijana kukaa bila kazi.

“Kijana anamaliza shule yake, anakaa na vyeti vyake kusubiri ajira ya serikali na hii ni kwa sababu hatujawatayarisha vya kutosha kujua stadi za kazi na kupata ule utaalam kwamba kazi zipo ni yeye kuchangamkia na kwenda kujiajiri. Hatuhangaiki kutafuta fursa za kazi, kazi ziko nyingi sana Tanzania, ni vijana kuchakarika kuziona hizo fursa na kuanza kuzitumia,” amesema Rais Samia.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments