WAKULIMA WATOA MAOMBI KWA KIONGOZI WA CCM


Mkurugenzi wa Nyanhembe Agricultural Farm Khamis Mgeja mwenye kofia ya kijani akifafanua jambo kwa Katibu wa itikadi na uenezi Mkoa wa Simiyu, George Mayunga kuhusu suala la changamoto inayowakabili wakulima wa kijiji cha Nyanhembe Kata ya Kilago Halmashauri ya Manispaa ya Kahama Mkoani Shinyanga.

Na Paul Kayanda, Kahama

BAADHI ya wakulima wa Kijiji cha Nyanhembe Kata ya Kilago Wilayani Kahama, Mkoani Shinyanga wameiomba Serikali kusambaza mbegu za mazao yanayostahimili ukame ili kuendana na mabadiliko ya tabia nchi.

Miongoni mwa mazao yanayotakiwa ni pamoja na mbegu za mtama mweupe, Mihogo, viazi pamoja na arizeti kulinga na msimu huu wa mvua za masika kunyesha kwa kusua sua.

Wakulima hao walitoa maombi hayo mbele ya katibu wa itikadi na uenzi Mkoa wa Simiyu,George Mayunga alipotembelea Kijiji hicho kwa lengo la kuwasalimia viongozi waliowahi kukitumikia chama na Taifa na kuona shughuli za kilimo katika mashamba ya mmoja wa viongozi hao, Khamis Mgeja aliyewahi pia kuwa mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga.

Mgeja pamoja na wakulima wengine walitumia fursa ya ujio wa kiongozi huyo kwenye mashamba yao kufikisha kilio chao na kumuomba kwamba afikishe maombi yao serikalini kwakuwa yeye ni kiongozi katika chama.

Mgeja ambaye ni mkurugenzi wa Nyanhembe Agricultural akiwasilisha changamoto za wakulima alimuomba katibu Mwenezi wa Mkoa kuwa afikishe maombi hayo kwa serikali ili iweke msukumo kwa wakulima kulima mazao yanayostahimili ukame.

“Sisi wakulima na wewe kama kiongozi tunakuomba ufikishe maombi yetu serikalini, kwamba ipo haja ya serikali kuweka msukumo wa kila kaya kulima kilimo cha mazao yanayostahimili ukame, hasa mtama pamoja na mihogo,” alisema Mgeja.

Pia mkurugenzi huyo wa Nyanhembe Agricultular Farm alishauri kuwa iwapo kila kaya italima shamba la angalau heka moja ya shamba la mtama hali ambayo itaodoa tatizo la njaa ambalo kwa sasa zao hilo la mtama litaendana na mabadiliko ya tabia nchi.

“Kwa hiyo tushirikiane, wananchi kuanzia viongozi wa serikali za vijiji hadi ngazi ya Taifa hasa wizara yenyewe ya kilimo chini ya Waziri wake mwenye dhamana Husein Bashe ili tusaidiane mawazo ya nini cha kufanya kuhusu kuwakomboa wakulima ili kuondokana na kilimo cha mazoea cha zao moja tu la mahindi,”alisema Mgeja.

Vile vile Mgeja alitumia nafasi hiyo kuwaomba viongozi wa dini kuendelea kuliombe Taifa ili lisije likakumbwa na Bala la Njaa kwamba kila mmoja aombe kwa Imani yake ama kufanya ibada ya Pamoja kumlilia Mungu ili kupata mvua nyingi na kunusuru bala la njaa kulikumba Taifa.

Naye Hatibu Mgeja Mkurugenzi mwenza wa Nyanhembe Agricultural Farm akizungumza kwa niaba ya wakulima wa Kijiji chake alisema kuwa kwa kipindi cha miaka miwili mfululizo iliyopita kumekuwa hakuna mvua za kutosha, hali ambayo wakulima wanakumbana na changamoto ya mazao kuharibika kutokana na mvua chache.

“Kama kiongozi wa chama tunakuomba, kupitia vikao vya chama na shughuli zote za kiserikali tunakuomba ufikishe kilio hiki kwa mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, kwani tunatamani sasa ifike wakati serikali ituchimbie hata mabwawa ambayo tunaweza kutumia kwa kilimo cha umwagiliaji Pamoja na kunywesha mifugo yetu,” alisema Hatibu Mgeja.

Mgeja aliongeza kuwa kama tunataka Taifa ambalo halina njaa umefika wakati wakulima wabadilishiwe mitazamo ili waache kulima kilimo cha mazoea, tuanze kutazama mazao amabayo hayana uhitaji wa mvua nyingi.

Hatua hiyo iliungwa mkono na wakulima wengine wa Kijiji hicho ambapo Felista Senga alisema kuwa kwa sasa wakulima wanalazimika kumwagilia baadhi muhimu kwenye mashamba yao hasa mahindi kulingana na dhana duni za kilimo na ukosefu wa mabwawa.

Senga anamwomba Rais Samia awaangalie hasa wanawake ambao ndiyo wahanga katika majanga mbalimbali hasa linapotokea balaa la njaa huwa ni wakwanza kubabaika na kuhangaika kwamba Watoto na familia zao wale nini wakati huo baadhi ya wababa hawajulikani waliko na inapelekea mpaka kutelekezewa.

“Tunamwomba mhe.Rais Samia suluhu Hassan atutazame sisi akina mama kwa macho mawili ili tupate vitendea kazi katika kilimo, mabwawa ya maji pamoja na pembejeo zikiwemo mbegu za mazao yanayostahimili ukame ili tumudu kuhudumia familia zetu,” alisema Senga.

Hata hivyo kwa upande wake katibu wa itikadi na uenezi Mkoa wa Simiyu George Mayunga akizungumza na wakulima hao katika Kijiji cha Nyanhembe aliwaahidi kufikisha maombi hayo pindi atakaporudi Simiyu na kwamba ataweka mawazo hayo katika vikao vya chama ili kuzungumza changamoto za wakulima kwa ujumla.

Katibu huyo alikili kuwa hali ya ukame inaweza kutokea iwapo mvua za masika zitagoma, huku akitumia mwanya huo kuwakumbusha kuwa mwishoni mwa mwaka jana mwenyekiti wa CCM Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan wakati wa maadhimisho ya miaka 50, ya hospitali ya Rufan kanda ya ziwa Mwanza.

Rais Samia wakati huo akiwa na viongozi wa Dini Taifa letu kwa kujua hali ya hewa hivyo Mh. Rais kwa kujua hilo alihamasisha na kuwasisitiza wananchi kuangalia hali ya hewa na kuwataka wananchi kulima mazao yanayostahimili ukame na muhimu Zaidi watanzania waendelee kufanya maombi.

Pia katibu Mwenezi alimpongeza sana aliyawahi kuwa mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM Mkoa wa Shinyanga, ikiwemo namaeneo ya Simiyu, Khamis Mgeja baada ya kupumzika siasa na kuamua kujielekeza katika shughuli za kilimo na kwamba hali hiyo ni kufuata nyayo za baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments