SERIKALI KUJA NA UTARATIBU WA KUSHIRIKISHA MAKAMPUNI MAKUBWA YA UMEME KUTOKA NJE YA NCHI KUTEKELEZA MIRADI YA REA


Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati vijijini Julias Kalolo

***
Na Dotto Kwilasa - Malunde 1 blog,Dodoma

WAZIRI wa Nishati nchini January Makamba amesema Serikali imepanga kuja na utaratibu mpya wa kushirikisha makampuni makubwa ya umeme kutoka nje ya nchi ili kutekeleza miradi ya Wakala wa umeme vijijini (REA) kwa haraka na ufanisi.

Waziri Makamba amebainisha hayo jijini Dodoma ,katika kikao chake na wafanyakazi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na kusema kuwa hali hiyo itabadilisha utendaji wa sasa wa kufanya miradi ya REA, ili kuongeza kasi ya utekelezaji na ufanisi.

“Najua kwa sasa utekelezaji wa REA utegemea fedha za mwisho wa mwezi, hatuwezi kusubiri hadi miaka 25 ijayo kukamilisha miradi hii, tunapamga kualika Makampuni makubwa duniani yanayoweza kufanya miradi mikubwa ya umeme",amesema.

Makampuni hayo kutoka nchi kama vile China ambako kuna kampuni zimefanya miradi ya umeme eneo kubwa kuliko hata Tanzania kwa haraka na ufasi lakini pia mengine ni ya kutoka Brazil ambao pia waliwahi kuwa shida kama yetu”,amesema Makamba.

Pamoja na hayo amesema serikali imepanga katika kipindi cha miaka minne ijayo kukamilisha kufikisha umeme katika vitongoji vyote 37,000 nchini vilivyobakia.

“Vitongoji 37,000 vimebaki kati ya vitongoji 64,000 nchini tunaweza kuvimaliza ndani ya miaka minne bila kusubiri fedha za mwisho wa mwezi, kwa kushirikisha wakandarasi ambao watakuja na fedha na sisi kuweka usimamizi kuhakikisha kuwa miradi hiyo inatekelezwa haraka na kwa ufanisi zaidi,"amesisitiza Waziri Makamba.

“Tunaweza kukubaliana na mkandarasi na kumpatia vitongoji 6,000 na tukaweka usimamizi mzuri tutapiga hatua kuliko ilivyo sasa, nategemea kabla ya mwisho wa mwezi Januri mwakani tutawaeleza nini tunataka kwenda kufanya na kwa uharaka zaidi hii habari ya nguzo imeanguka,transifoma feki tunaachana nayo”amesisitiza.

Waziri huyo pia ameutaka uongozi wa REA, kusimamia utaratibu na miongozo ya sheria ya manunuzi ya umma ambayo imekuwa ikilalamikiwa na watu wengi katika Wakala huo.

“Zingatieni utarabu wa manunuzi unatia doa wakala wenu naomba muuweke sawa tusijefika sehemu tukaonana wabaya haiwezekani suala la mtu kupata tenda REA waziri nasumbuliwa na watu kutaka niwape upendeleo mimi mambo haya sijazoea naomba utaratibu huu muufanyie utaratibu kabla hatuja onana wabaya,

Nawataka,nawaelekeza,nawasihi suala hili tulitizame vizuri litawatia doa na tukifika huko hatutakuwa na mswalia mtume”amesema

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati vijijini Julias Kalolo, ametumia nafasi hiyo kumshukuru waziri huyo kwa kutenga muda wa kuzungumza na watumishi wa wakala huo kwa mara ya kwanza toka ashike wadhifa huo.

"Tunashukuru sana,tunaahidi kufuata maelekezo yote uliyotupatia, tutahakikisha wananchi wanapata huduma bora na kukuza uchumi ikiwa ni pamoja na kuwaondolea wananchi vijijini kero ya umeme,"amesema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments