MAKAMU WA RAIS, DKT. MPANGO AZINDUA MNARA WA MAWASILIANO KIJIJI CHA KASUMO, KIGOMA


Mhe. Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdori Mpango akikata utepe kuashiria Uzinduzi wa Mnara wa Mawasiliano katika Kijiji cha Kasumo Kata ya Kajana Wilaya ya Buhigwa mkoani Kigoma. Kulia kwa Makamu wa Rais ni Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) huku kushoto kwake ni Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Tanzania, Bw. Waziri Kindamba.
Mhe. Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdori Mpango akisalimiana na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Bw. Waziri Kindamba wakati wa Uzinduzi wa Mnara wa Mawasiliano katika kijiji cha Kasumo Kata ya Kajana Wilaya ya Buhigwa Mkoani Kigoma.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Tanzania, Bw. Waziri Kindamba (kulia) akipata picha ya kumbukumbu katika uzinduzi huo.
Mhe. Makamu wa Rais, Dkt. Philip Isdori Mpango akiwapungia mkono wananchi wa Kijiji cha Kasumo na Vijiji jirani waliofika kushuhudia Uzinduzi wa Mnara wa Mawasiliano katika Kijiji cha Kasumo Kata ya Kajana Wilaya ya Buhigwa Mkoani Kigoma.
Mhe. Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdori Mpango akiwapungia mkono wananchi wa Kijiji cha Kasumo na Vijiji jirani waliofika kushuhudia Uzinduzi wa Mnara wa Mawasiliano katika kijiji cha Kasumo Kata ya Kajana Wilaya ya Buhigwa Mkoani Kigoma.
Mhe. Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isdori Mpango akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Kasumo na Vijiji jirani waliofika kushuhudia Uzinduzi wa Mnara wa Mawasiliano katika kijiji cha Kasumo Kata ya Kajana Wilaya ya Buhigwa Mkoani Kigoma.

Na Adeline Berchimance, KIGOMA

SERIKALI itaendelea kuweka mazingira mazuri na uwekezaji katika Sekta ya Mawasiliano ili iweze kutoa mchango mkubwa zaidi katika kuchochea shughuli za maendeleo.

Hayo yamebainishwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Mpango alipokuwa akizindua mnara wa Mawasiliano katika Kijiji cha Kasumo Kata ya Kajana Wilaya ya Buhigwa mkoani Kigoma.

Alisema mnara huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali ya Awamu ya Sita wa kuhakikisha huduma za mawasiliano zinapatikana nchi nzima na kwa gharama nafuu ili kuwawezesha wananchi wanaoishi pembezoni na hasa vijijini waweze kumudu matumizi ya huduma hiyo.

Alisema ujenzi wa mnara katika Kijiji cha Kasumo ni mwendelezo wa jitihada za Serikali kuufungua Mkoa wa Kigoma na kuwezesha wananchi kutumia huduma za intaneti, ambazo pia zitaboresha huduma za kijamii na kufungua fursa za kiuchumi.

Mhe. Dkt. Mpango amewaeleza wananchi fursa zitakazopatika kutokana na matumizi ya intaneti na mawasiliano ya simu kwa ujumla ni pamoja na kuwaunganisha wananchi wa Kata ya Kajana, Kata ya Muyamba na Vijiji jirani, pia kuunganishwa na masoko ya mazao yanayozalishwa katika Wilaya hiyo na biashara mbalimba zinazofanyika katika Wilaya hiyo.

“Mtandao wa simu unatuwezesha kuongeza na kupanua mtandao wa Wateja na hivyo kurahisisha shuguli mbalimbali za kiuchumi,” alisema Dkt. Mpango.

Aidha amebainisha kuwa kupitia mnara huo wananchi wataweza kuwasiliana moja kwa moja na vyombo vinavyotoa huduma muhimu za kijamii, pamoja na kupata ushauri kutoka kwa wataalam wa kilimo, ufugaji na kuboresha shughuli zao, huku Wanafunzi wa Shule za Msingi hadi vyuo kunufaika pia kwa matumizi ya intaneti kujisomea na kujipatia maarifa mapya.

Kwa kuzingatia faida na fursa zinazopatikana katika huduma ya mawasiliano, Dkt. Mpango amewataka wananchi wa Kijiji cha Kasumo na Wilaya nzima ya Buhigwe kulinda na kutunza miundombinu hiyo kwani imegharimu fedha nyingi za Serikali.

Amesema uharibifu wa miundombinu hiyo italeta hasara na madhara makubwa kwa wananchi wa Buhigwe na Kasulu kiuchumi na kijamii

“Ukiharibiwa huu mtambo maana yake tutakosa huduma ya mawasiliano pamoja na faida zote za huduma hii zitapotea na hivyo kurudisha nyuma juhudi za serikali za kuwaletea maendeleo,” alisema  Dkt. Mpango.

Aidha amewataka Wanachi hao kutumia vyema huduma hii na kujiepusha na matumizi mabaya ya mitandao ikiwemo kutazama na kusambaza picha ambazo hazina maadili kulingana na tanaduni za kitanzania.

Kwa upande wake Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) amelipongeza Shirika la Mawasiliano -TTCL kwa kushirikiana na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote –UCSAF kwa kufikisha huduma ya mawasiliano ya uhakika kwa wakazi wanaoishi katika kijiji cha cha kasumo pamoja na vijiji jirani.

Amesema mnara huo utatoa huduma ya Intaneti kwa kazi ya 4G ambayo imekuwa ni hitaji msingi kwa maisha ya mwanadamu katika dunia ya sasa na kwamba mnara huo unaenda kufanikisha agenda ya serikali ya kufikisha huduma ya intaneti hadi ngazi ya vijiji.

Alisema pamoja na ujenzi wa mnara huo Wizara yake ipo katika mkakati wa kufikisha Mkongo wa Taifa mpaka Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe katika kipindi cha mwaka huu wa fedha.

Alisema Mkongo huo utarahisisha Zaidi huduma ya intaneti zilizofikishwa na mnara huo kwa bei nafuu Zaidi kwa wananchi wa Wilaya ya Buhigwe na Kigoma nzima ili kujenga uchumi wa kidigitali.

Alisema Mradi huo uliozinduliwa ni sehemu ya miradi ya mawasiliano vijijini inayotekelezwa kupitia mfuko wa Mawasiliano kwa Wote ambapo mpaka sasa TTCL kwakushirikiana na UCSAF imeishajenga minara  katika Kata 171 zinazojumuhisha vijiji 381.

Alisema TTCL imeendelea kubeba dhamana ya usimamizi na uendeshaji wa miundo mbinu ya kimkakati ya mawasiliano, kiufundi na kibiashara ikiwemo Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano na Kituo Mahili cha Kuhifadhi Data yaani.

Alisema miundo mbinu hii imekuwa na matokeo chanya kwenye maendeleo ya Taifa ambapo mpaka sasa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano umefika katika nchi zilizoko katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika.

Akisoma taarifa ya Mradi wa Mnara huo Mkurugenzi Mkuu Shirika la Mawasiliano Bw. Waziri Kindamba alisema mradi huo umekamilika katika kipindi cha miezi miwili huku ukigharimu shilingi 326,874,773.75.

Bw. Kindamba alisema TTCL imetoa shilingi 208,624,772.75 huku Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) ikitoa kiasi cha shilingi 118,250,000.00.

Alisema mnara huo una uwezo wa kutoa huduma za mawasiliano ya Intaneti, Ujumbe Mfupi na Dakika (Voice) kwa teknolojia ya kisasa ya 4G, kubwa zaidi wananchi watapata fursa ya kutumia huduma za Intaneti yenye kasi zaidi.

Alisema kuwa huduma hii ya mawasiliano italeta mageuzi makubwa katika Kata ya Kajana kutokana na uwepo wa fursa mbalimbali kiuchumi na kijamii ikiwemo kuondoachangamoto ya Mawasiliano na kufungua fursa za kiuchumi kwa wananchi kuweza kujipatia kipato kupitia uwakala wa huduma mbalimba za TTCL na Kampuni tanzu ya T-PESA.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, Bi Justina Mashiba alisema jukumu kubwa la Taasisi yake nikuhakikisha wananchi wanaoishi maeneo ya vijijini na mipakani mwa nchi wanapata huduma za mawasiliano.

Alisema UCSAF imejipanga vizuri kuhakikisha kila Mtanzania anayeishi Kijijini au maeneo ya pembezoni anapata huduma za mawasiliano.

“maeneo ya mipakani ni sehamu ambazo zinahitajika kulindwa kwa ajili ya usalama wa nchi yetu hivyo ni jukumu la UCSAF kuhakikisha maeneo hayo yanalindwa na Watanzania wanaishi na kufanya shughuli zao katika maeneo hayo wanapata huduma za mawasiliano,” Alisema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments