MWILI WA MFANYABIASHARA WA MADINI ANAYEDAIWA KUUAWA NA MWANAE WA KUMZAA WAZIKWA ARUSHA



Ruth Mmasi enzi za uhai wake

MFANYABIASHARA wa madini ya Tanzanite, Ruth Mmassy anayedaiwa kuuawa na mtoto wake amezikwa leo Jumatatu Desemba 27, 2021 katika kijiji cha Mikungani, Wilayani Arumeru, Mkoani Arusha.

Akiongoza ibada ya mazishi Mchungaji wa Kanisa la Kiijili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Mikungani, Ernest Mola amesema wanasikitishwa na tukio hilo kwani marehemu alikuwa mtu wa kujitolea.

“Mara ya mwisho alichangia usharika Sh1 milioni na tukashukuru kwa namna alivyojitolea kwa Mungu” amesema Mchungaji.

Kaka wa marehemu Hamis Mmassy amedai tamaa za mali ndizo zimesababisha mtoto huyo kumuua mama yake.

“Marehemu hakuwa anaumwa alikuwa mzima wa afya ndiyo hivyo kama ulivyosikia kuwa mtoto wake wa kumzaa amemuua mama yake,” Mmassy.

Mwenyekiti wa kijiji cha Mikungani, mwalimu Issa Salum amesema Ruth alisoma shule ya msingi Mikungani na alimfundisha kipindi akiwa mwalimu.

Kwa upande wa Mwenyekiti wa madalali wa madini mkoani humo, Jeremia Simon amesema Ruth alizaliwa mwaka 1985 kwenye kitongoji cha Kairo mji mdogo wa Mirerani.

Simon amesema marehemu alipotea kwenye Mazingira ya kutatanisha Desemba 11 mwaka huu na kugundulika amefariki Desemba 24 saa 8 mchana Njiro Contena jijini Arusha.

Kamanda wa Polisi Mkoa Arusha Justine Masejo amesema Polisi bado wanamshikilia Mtoto wa marehemu Patrick Mmassy( 19) kwa uchunguzi wa tukio Hilo la mauwaji.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments