IHOMBWE WAMSHUKURU DC KURUHUSU UJENZI WA DARASA NA NYUMBA YA WAUGUZI


Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Ihombwe, Mikumi wilayani Kilosa Vashty Chimwile akitoa taarifa kuhusu Usimamizi Shirikishi wa Misitu katika kikao kilichofanyika kijini hapo wakati waandishi wa habari walipotembelea kukagua shughuli za usimamizi wa misitu.
Baadhi ya wanakamati wa Ulizni Shirikishi wa Misitu katika kijiji cha Ihombwe wilayani Kilosa mkoani Morogoro wakiwa katika kikao hicho.
Na Mwandishi Wetu

WAKAZI wa kijiji cha Ihombwe kilichopo katika Mamlaka ya Mji mdogo wa Mikumi, Kilosa, mkoani Morogoro, wamemshukuru Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Majid Mwanga, kwa kuruhusu pesa zao zilizoko benki, takribani Sh milioni 70 kutumika kwa ajili ya ujenzi wa madarasa katika Shule ya Msingi ya Kijiji.

Pesa hizo zilizopatikana kutokana na mradi wa Usimamizi Shirikishi wa Misitu ya Jamii (USMJ) hususani uvunaji wa mabo, zitatumika pia kujenga nyumba kwa ajili ya wauguzi. 

Ofisa mtendaji wa kijiji hicho, Vashti Chimile, alisema awali Mkuu huyo wa Wilalaya alizuia fedha hizi zisifanye lolote mpaka atakapotoa maelekezo na yeye alitaka zitumike kwa kujenga Shule ya Sekondari ya kijiji kwani kwa sasa kijiji hicho hakina shule ya sekondari.

Uamuzi huo wa kuanza kwa kujenga sekondari, ulikuwa kinyume na uamuzi wa wanakijiji ambao waliona kipaumbele kikubwa ni darasa la kwanza ambalo ni bovu likitishia uhai wa wanafunzi pamoja na kuwaondolea adha wauguzi wa zahanati ambao hawana makazi na wakati mwingine hulazimika kulala ndani ya zahanati. 

Kupitia mapato ya misitu, wakazi wa kijiji hicho tayari walishajenga nyumba ya Mganga wa zahanati ambaye huko nyuma alikuwa akilazimika kuishi katika mji wa Mikumi, umbali wa takribani kilometa 20.

“Tunasmhukuru sana Mkuu wa Wilaya kupitia kwa diwani wetu kuruhusu tufanye matumizi kwa kufuata sheria taratibu na kanuni… Tutaanza na darasa katika Shule ya Msingi Ihomnbwe, kisha nyumba ya wauguzi na ndipo tutanza kujenga shule ya sekondari.” Kijiji cha Ihombwe hakina shule ya sekondari na wanafunzi wanaofaulu hupelekwa katika shule za sekondari zilizo katika mji mdogo wa Mikumi. 

“Kutokana na umbali na shule zile si mabweni watoto hukazimika kupanga, tunaita ghetto lakini changamoto kubwa inakuwa ni kwa wasichana,” alisema Mtendaji huyo. Alitoa mfano kwamba mwaka jana, watoto 44 wa shule ya msingi ya kijiji walifaulu lakini wasichana 10 hawajenda shule na wawili wameishia njiani.

Mwenyekiti wa zamani wa kijiji hicho, Philemon Robert, alishukuru uamuzi wa Mkuu wa Wilaya kuruhusu waanze ujenzi kwa kufuata uamuzi wa wanakijiji kwa maana ya kuanza darasa katika shule ya msingi na nyumba ya wauguzi.

“Kwa kweli kama angesimamia uamuzi wake kwamba tuanza na sekondari ingawa tunaihitaji sana, sisi wanakijiji tungerudi nyuma kidogo kwa sababu tatizo la haraka kwetu ni darasa kwa ajili ya watoto wa darasa la kwanza kwa saababu lililopo lina nyufa, linaweza kuanguka muda wowote na pili ni nyumba za wauguzi.”

Mwaka 2012 kijiji hicho kilipokea mradi wa kuleta mageuzi katika sekta ya mkaa Tanzania maarufu kama Mkaa Endelevu ambao ulikifanya kutoka katika mapato chini ya laki moja kwa mwakahadi kufikia wastani wa shilingi milioni 33 kwa mwaka.

Mradi wa Mkaa Endelevu unaojikita katika Usimamizi Shirikishi wa Misitu unaanza kwa kijiji kupima mipaka na kuwa na matumizi bora ya ardhi kwa kutenga eneo la makazi, mashamba na msitu

Eneo linalotengwa kwa ajili ya mkaa ni asilimia 10 mpaka 15 tu maisha yote na linavunwa kwa kuruka ruka. Kwa mfano msitu wa kijiji hicho una ukubwa wa hekta 9,597 lakini eneo lilolotengwa kwa ajili ya mkaa ni hekta 2,724,5.

Hata hivyo, mapato ya kijiji hicho yamerudi nyuma sana kutokana na tangazo la serikali namba 417 lililoondoa madaraka ya vijiji kujipangia tozo za ushuru. Serikali imekuwa ikiombwa kutembelea vijiji vyenye miradi hiyo na kusikiliza wananchi ili kuangalia upya madhara ya tangazo hilo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments