WAZIRI MKUMBO ATEMBELEA KIWANDA CHA VIFAA VYA UMEME 'AFRICABLE'....ATAKA WATANZANIA KUTHAMINI BIDHAA ZA NDANI

WAZIRI wa Viwanda na Biashara Profesa Kitila mkumbo amekipongeza kiwanda cha utengenezaji wa vifaa vya umeme cha Kilimanjaro Cables (AFRICABLE) kwa kuzalisha vifaa vya umeme vyenye ubora huku akiwataka watanzania kuona haja ya kutumia vifaa vinavyozashwa hapa nchini.

Akizungumza mara baada ya ziara yake ya kutembelea viwanda vya uzalishaji wa transfoma, nyaya na vifaa confine vya umeme vinavyomilikiwa na kampuni hiyo Waziri Mkumbo alisema haoni haja ya kuagiza vifaa vya umeme kutoka nje ya nchi kwa kuwa kwa sasa viwanda vya ndani vina uwezo wa kuzalisha vifaa hivyo vinavyotosheleza mahitaji ya watanzania na vingine kuuzwa nje ya nchi ikiwemo transfoma.

Alisema nia ya Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan ni kuona viwanda vya ndani vinazidi kuwa vyenye nguvu na ubora katika uzalishaji ili kuleta ushindani na viwanda vya nje jambo ambalo pamoja na mambo mengine litasaidia kulitangaza taifa.

"Nimetembelea viwanda hivi na kujionea hali halisi ilivyo hasa kuhusu uzalishaji, natambua changamoto zilizopo kwenye bidhaa za ndani ikiwemo suala la kodi na masoko, Serikali inakwenda kutatua haya yote kwa lengo la kuvipa nguvu zaidi viwanda vyetu vya hapa nchini" ,alisema Profesa Mkumbo.

Alisema uwekezaji wa kiwanda hicho, mbali na kuipunguzia Serikali mzigo wa gharama, pia umesaidia kuharakishwa kwa utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme nchini ikiwemo ya REA hatua inayoendelea kuliletea maendeleo Taifa na hivyo kusisitiza haja ya wawekezaji hao kuendelea kuthaminiwa.

Aidha Profesa Mkumbo alisema kwa kuwa serikali inatambua mchango mkubwa wa mwekezaji huyo na mkakati wake wa ujenzi wa mtaa maalumu la uwekezaji wa viwanda vyake vyote katika eneo moja huko Kimbiji Kigamboni, wataboresha miundombinu katika wilaya ya kigamboni ili kurahisisha mazingira yote ya kufika eneo hilo.

Kwa upande wake Meneja Masoko kutoka Kilimanjaro Cable(AFRICABLE) David Tarimo alisema wataendelea kuzalisha bidhaa zenye ubora na zinazokidhi mahitaji ya watanzania ili kutimiza malengo ya Serikali ya kuwa na viwanda bora kwa uzalishaji wa bidhaa mbalimbali.

Alisema wao kama wawekezaji wazalendo wa hapa nchini jukumu lao ni kuhakikisha wanaendelea kushirikiana na Serikali kuhakikisha sekta ya nishati nchini inakuwa yenye tija kwa kuzalisha bidhaa zenye ubora zitakawawezesha wananchi kuzitumia kwa muda mrefu.

Alisema changamoto wanayokabiliana nayo ni baadhi ya wananchi kuendelea kuamini bidhaa zinazozalishwa nje ya nchi ambazo nyingi zimekuwa zikiingizwa kwa njia ya panya na zaidi zikikosa ubora ikilinganishwa na bidhaa zinazozalishwa nchini.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Prof Kitila Mkumbo akizungumza na waadishi wa Habari  jijini Dar es Salaam baada ya kufanya ziara katika viwanda vya Africab vilivyopo kiwalani na Kurasini vinachozalisha Transfoma, Nyaya na vifaa vya umeme.Waziri ameambatana na Wakurugenzi wa Kiwanda hicho, Aliagha Ezzi (wa tatu kushoto) Yusuf Ezzi na Mansoor Moiz. 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments