SAMIA ATAKA WANAWAKE WAJIPANGE URAIS 2025

Rais Samia Suluhu Hassan amewataka wanawake kujipanga kuhakikisha wanaweka Rais mwanamke katika Uchaguzi Mkuu ujao.

Vilevile, amehoji kilichoandikwa na moja ya gazeti nchi kwamba hana nia ya kuwania urais mwaka 2025, akiuliza 'nani kawaambia?'

Rais Samia alitoa kauli hiyo jana jijini Dar es Salaam katika maadhimisho ya Siku ya Demokrasia Duniani yaliyohudhuriwa na taasisi mbalimbali na wasichana 50 ambao waliokolewa kwenye biashara ya usafirishaji wa binadamu.
 
Katika maadhimisho hayo, Rais Samia alikabidhiwa tuzo tatu, moja ikitolewa na Mwenyekiti wa Azaki ya Wanawake Tanzania (Ulingo), Anna Abdallah, ya pili kutoka kwa watoto waliookolewa katika udhalilishaji wa kimaisha na nyingine kutoka kwa masista wa St. Joseph.
 
Akizungumza katika maadhimisho hayo, Rais Samia alisema, “Leo (jana) mmempa tuzo Rais wenu, Rais mwanamke, kwa bashasha na furaha kubwa, lakini ninataka niwaambie wanawake bado hatujaweka Rais mwanamke.
 
Rais Samia alifafanua kuwa Rais huyo mwanamke amekaa kwa sababu ya kudra ya Mwenyezi Mungu na matakwa ya Katiba.
 
“Tulichokichangia sisi na dada zetu na mama zetu na Mama Anna Abdallah ni ile kusukuma mpaka mwanamke akawa Makamu wa Rais, ule ndio mchango mkubwa ambao tumeufanya wanawake.
 
"Kama isingekuwa mpango wa Mungu, ingekuwa ngumu, tungefikia hapo kila mwaka tunakwenda ni hapo, ni hapo," alisema.
 
Rais Samia aliwaeleza kuwa Rais mwanamke watamweka mwaka 2025.
 
“Mwaka 2025 wanawake tukifanya vitu vyetu vizuri, kushikamana, tukimweka Rais wetu, tutakutana hapa kwa furaha kubwa sana. Wameanza kutuchokoza, wameanza kutuchokoza kuandika kwenye vigazeti 'Samia hatasimama', nani kawaambia?
 
“Fadhila za Mungu zikija mikononi kwako usiziachie, hizi ni fadhila za Mungu ndugu zangu, wanawake tumefanya kazi kubwa kuleta uhuru wa nchi hizi, wanawake tumefanya kazi kubwa kujenga siasa za nchi, tumebeba sana wanaume katika siasa za nchi hizi.
 
"Leo Mungu ametupa baraka mikononi, tukiiachia Mungu atatulaani," alisema huku ukumbi ukilipuka kwa shangwe.
 
Machi 19, mwaka huu, Samia ambaye alikuwa Makamu wa Rais, aliapishwa kuwa Rais wa nchi kutokana na kifo cha Rais wa Awamu ya Tano, Dk. John Magufuli, suala hilo lilifanyika kwa mujibu wa Katiba.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments