NFRA YANUNUA TANI 4,600 ZA MAHINDI YA WAKULIMA RUKWA


Sehemu ya vihenge vya kisasa sita vyenye uwezo wa kuhifadhi tani 20,000 vinavyojengwa na serikali kwa ajili ya kuongeza uwezo wa NFRA na kuhifadhi nafaka kwa Kanda ya Sumbawanga. (Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Rukwa).
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe. Joseph Joseph Mkirikiti (kushoto) akiwa kwenye mazungumzo na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Bw. Milton Lupa leo alipofika Sumbawanga kwa ziara ya kikazi kukagua mwenendo wa ununuzi wa mahindi ya wakulima.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe. Joseph Joseph Mkirikiti (kushoto) akiwa kwenye mazungumzo na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Bw. Milton Lupa (kulia) leo alipofika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo mjini Sumbawanga kwa ziara ya kikazi kukagua mwenendo wa ununuzi wa mahindi ya wakulima.
**

Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula nchini (NFRA) imefanikiwa kununua tani 4,600 za mahindi zenye thamani ya Shilingi Bilioni Mbili na Milioni Mia tatu ( 2,300,000,000) toka kwa wakulima kati ya lengo la tani 5,000 zilizopangwa awamu ya kwanza kufikia Agosti 31, mwaka huu.

Hayo yamebainishwa leo (01.09.2021) wakati Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Milton Lupa alipokutana na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti ofisini kwake Sumbawanga akiwa katika ziara ya kukagua zoezi la ununuzi wa mahindi Meupe linaloendelea katika Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini.

Lupa aliongeza kusema serikali inaendelea kuweka mazingira wezeshi ili kuendelea kununua mahindi ya wakulima kulingana na upatikanaji wa fedha.

“Wakala unaendelea kufuatilia fedha toka Serikalini ili itekeleze jukumu la kununua mahindi ya wakulima kama ilivyopangwa kwenye bajeti ya mwaka 2021/2022 hivyo wananchi wa Rukwa wawe na subira” alisema Lupa.

Lupa aliongeza kusema Wakala unaendelea kukamilisha ujenzi wa vihenge vya kisasa na kuwa lengo mahindi yote yatakayonunuliwa Rukwa msimu huu yahifadhiwe .

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joseph Mkirikiti alisema wananchi wa Rukwa wamezalisha kwa wingi mahindi kwa kuwa ni zao lao la biashara hivyo wanategemea zaidi NFRA kama soko la uhahika.

“Tunaendelea kuiomba serikali itupatie mgao zaidi sisi wana Rukwa kwani zao letu la mahindi ndio zao la biashara kwa wananchi wengi” alisisitiza Mkirikiti.

Kwa mujibu wa takwimu za uzalishaji wa mazao ya chakula kilimo msimu wa 2020/2021 mkoa wa Rukwa ulizalisha tani 651,433 za mahindi kati ya lengo la tani 731,500 ambapo kutokana na uzalishaji mkubwa mkoa una ziada ya mahindi tani 354,117.

Mwisho.

Imeandaliwa na;

Afisa Habari Mkuu,

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Rukwa,

SUMBAWANGA

01.09.2021

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments