HESLB YAONGEZA MUDA WA SIKU 15 UOMBAJI MIKOPO, WALIOPO JKT KUPEWA FURSA HADI SEPTEMBA 30

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), Abdul-Razaq Badru akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari uliofanyika leo Jumatano Septemba 1, 2015. Katika mkutano huo HESLB ilitangaza kuongeza muda wa siku 15 kwa waombaji mikopo kuanzia Septemba 1-15 mwaka huu.
Mwakilishi wa Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA), Beatrice Mboya akizungumza na waandihi wa habari uliofanyika leo Jumatano Septemba 1, 2015. Katika mkutano huo HESLB ilitangaza kuongeza muda wa siku 15 kwa waombaji mikopo kuanzia Septemba 1-15 mwaka huu.
Mwakilishi wa Kaimu PostaMasta Mkuu wa Shirika la Posta Tanzania (TPC), Mbarouk Issa akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari uliofanyika leo Jumatano Septemba 1, 2015. Katika mkutano huo HESLB ilitangaza kuongeza muda wa siku 15 kwa waombaji mikopo kuanzia Septemba 1-15 mwaka huu.

 

Dar es Salaam, Septemba 1, 2021

 

Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imeongeza muda wa uombaji mikopo kwa siku 15 zaidi kuanzia Septemba 1 hadi 15 mwaka huu ili kuwapa fursa kwa waombaji mikopo ambao wamejisajili katika mfumo kukamilisha maombi yao.

 

Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Abdul-Razaq Badru ametangaza uamuzi huo leo (Jumatano, Septemba 1, 2021) jijini Dar es salaam na kufafanua kuwa uamuzi huo umetokana na maombi na ushauri walioupokea kutoka kwa wadau.

Idadi ya waombaji

“Tulianza kupokea maombi kwa njia ya mtandao Julai 9, mwaka huu na hadi jana ambayo ilikua siku ya mwisho ya kuomba tulikua na waombaji 91,445 waliowasilisha maombi, na kati ya hayo, maombi 12,252 yalikua hayajakamilika na wateja wetu wameomba muda wa kukamilisha,” amesema Badru.

Mkurugenzi Mtendaji alikua akiongea katika mkutano na wanahabari uliofanyika katika ofisi za HESLB jijini Dar es salaam ambao pia ulihudhuriwa na wawakilishi kutoka Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) na Shirika la Posta Tanzania (TPC) ambao pia wanawahudumia waombaji mkopo.

Hatua inayofuata

Kwa mujibu wa Badru, hatua inayofuata ni uhakiki wa nyaraka na taarifa zilizowasilisha na waombaji 79,193 ambao maombi yao yamekamilika kama yanavyoonekana kwenye mfumo.

“Kuna makundi mawili, wale 12,252 ambao maombi hayana viambatisho na hivyo hayajakamilika … na kuna maombi 79,193 yenye nyaraka, sasa tunaanza kuhakiki usahihi wake na baadae tutaangalia kama wamepata udahili na wale wenye sifa ndiyo watapangiwa mkopo,” amesema Badru.

Fursa ya kuomba mkopo vijana waliopo JKT

Kuhusu wanafunzi wahitaji wanaoendelea na mafunzo katika Kambi za Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Badru amesema vijana hao waliopo katika kambi 19 nchini watapata fursa ya kuomba mkopo kwa siku 10 kuanzia Septemba 20 hadi 30 mwaka huu.

“Tumekuwa tukiwasiliana na Makao Makuu ya JKT, na tumekwenda na kukutana na vijana hao katika kambi zote na tuliwaahidi kuwa watapata fursa … ambayo ni kuanzia Septemba 20 hadi 30 mwaka huu, hivyo wasiwe na wasiwasi,” amesema Badru.

RITA na TPC kuendelea kuwahudumia waombaji

Wakizungumza katika Mkutano huo, Mwakilishi wa Kaimu PostaMasta Mkuu, Mbarouk Issa amesema hadi TPC itaendelea kuhudumia wanafunzi waombaji mikopo wanaoendelea kutuma fomu za maombi katika Ofisi zozote za TPC zilizopo katika Mikoa na Wilaya zote nchini.

Kwa mujibu wa Mbarouk, hadi kufikia jana, Agosti 31, 2021 TPC ilikua imepokea fomu za wanafunzi 56,140 na nyingine 2,200 zikiwa njiani kufikishwa HESLB na kuwa TPC imejipanga kuendelea kuwahudumia wateja hao katika muda wote ulioongezwa.

Naye Mwakilishi wa Mtendaji Mkuu wa RITA, Beatrice Mboya amesema kupitia mfumo wa E-Huduma, RITA, imepata mafanikio makubwa na itaendelea kuhakiki vyeti vya kuzaliwa vya wanafunzi waombaji mikopo hadi dirisha hilo litakapofungwa ili kuweza kuwasaidia wateja kuweza kukamilisha na kuwasilisha maombi yao kwa usahihi.

“RITA ni wadau wakubwa wa masuala ya mikopo ya wanafunzi, kupitia mifumo yetu ya ndani tumepata mafanikio makubwa kwa kuhakiki maombi ya uhakiki wa vyeti vya wanafunzi, ambapo kati ya maombi 111,751 tumeweza kuhakiki vyeti vya kuzaliwa 111,358” amesema Mboya.

Bajeti ya mikopo kwa 2021/2022

Katika mwaka wa masomo 2021/2022, Serikali imetenga kiasi cha TZS 570 Bilioni kwa ajili ya kugharamia mikopo ya wanafunzi 160,000 wa taasisi za elimu ya juu. Kati ya hao, wanafunzi 62,000 wanatarajiwa kuwa ni wa mwaka wa kwanza na wanafunzi 98,000 wanaoendelea na masomo. Bajeti kwa mwaka 2020/2021 ilikua TZS 464 bilioni na zimewanufaisha jumla ya wanafunzi 149,398.

Imetolewa na:

 

Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu,

Dar es salaam, Jumatano, Septemba 1, 2021

Taarifa hii pia inapatikana katika www.heslb.go.tz

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments