MO DEWJI: HANS POPE ALIKUWA NA WEMA WA KIPEKEE



Na Emmanuel Mbatilo - Dar es salaam
Wanamichezo nchini wamepokea kwa masikitiko kwa kifo cha Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa klabu ya Simba, Zacharia HansPope ambaye amefariki dunia usiku wa kuamkia leo katika hospitali ya Aghakhan Jijini Dar es Salaam alipokuwa anapatiwa matibabu.

Viongozi mbalimbali wa michezo wameshindwa kujizuia na kutamka ya moyoni kuhusu umuhimu wa kiongozi huyo katika tasnia ya michezo hapa nchini.

Licha ya kuwa kiongozi wa klabu ya Simba alikuwa mtu wa hamasa katika kuitangaza tasnia ya michezo kwa taifa kwa ujumla.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Mohammed Dewji amesema Hans Pope alikuwa ni mtu wa kipekee alihakikisha klabu ya Simba kusonga mbele na alijali maslahi ya klabu.

“Nimefanya kazi na wewe kwa miaka mingi, na kila siku uliweka maslahi ya Simba mbele. Kaka yangu ulikua na wema wa kipekee, na ulikua wa kwanza na ulinyooka linapokuja suala la kuilinda Simba, hukuwa na maslahi binafsi. Ulikua rafiki wa marafiki wa Simba, na ulikua tofauti na wasioitakia mema Simba.” Amesema Mo Dewji

Kwa upande wake Mwenyekiti wa klabu ya Simba Murtaza Mangungu amesema Hans Pope alikuwa anapenda umoja na mshikamano kwa wanasimba wote kwani alikuwa anapenda mafanikio kwa ujumla ndani ya klabu.

“Ninamfahamu kwa miaka mingi akiwa ni Mwana Simba mahiri , mwenye msimamo na ukweli. Ni mtu aliependa umoja na kupata mafanikio kwa jumla. Siku zote alikubali kutumikia klabu kwa moyo wake wote , bila kujali muda wake, mali au hasara”. Amesema Mangungu

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments