MMOJA AFARIKI, 50 WANUSURIKA KIFO KWA KULA CHAKULA KINACHODAIWA KUWA NA SUMU KWENYE SHEREHE SINGIDA



Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge  akiwasalimia  na kuwapa pole manusura wa chakula  kinachosadikika kuwa na sumu.
Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge  akiwasalimia  na kuwapa pole manusura wa chakula  kinachosadikika kuwa na sumu.


Na Edina Malekela,Singida
Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge amewatembelea wananchi waliolazwa katika Hospitali ya Mkoa huo baada kula chakula kinachosadikika kuwa na sumu ambapo katika tukio mtoto mmoja  mwenye umri wa miaka 7 amefariki dunia huku watu wengine 50 wakinusurika kifo.

Wakazi hao wa Kata ya Unyambwa kijiji cha Kisasida katika Manispaa ya Singida mkoani Singida walifikishwa hospitalini hapo jana baada ya hali zao kuwa mbaya kutokana na kula chakula kilichoandaliwa katika shughuli za ufunguzi wa Madrasa kijijini hapo.

Dkt. Mahenge amewapongeza madaktari wa Hospitali hiyo kwa jitihada za kuhakikisha wananusuru maisha ya wananchi hao ambapo kwa sasa hali zao zinaendelea vizuri na kuipongeza Serikali kwa kuweka miundombinu mizuri ya huduma katika sekta ya afya.

Ametoa wito kwa Viongozi wa Serikali na Dini kuwajibika kikamilifu katika kutoa elimu ya namna ya kuandaa chakula pamoja na kusimamia inapotokea sherehe mbalimbali kwenye maeneo yao ili kuepuka madhara ya namna hiyo.

Kwa mujibu wa Mganga mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa Banuba Deogratius amesema walipokea jumla ya wagonjwa 50,kati yao Wanawake 34 na Wanaume 16 ambapo hali zao zinaendelea vizuri na wanaanza kuwaruhusu baadhi yao kurudi nyumbani kuendelea na majukumu yao.

Aidha Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Singida Stella Mutabihirwa amesema wanawashikilia washukiwa 7 walioshiriki kuandaa chakula hicho kwa ajili ya uchunguzi na tayari wamechukua chakula hicho kwa uchunguzi zaidi.

Katika tukio hilo Kamanda amesema mtoto mmoja mwenye umri wa miaka (7) ambaye amefahamika kwa jina la Fahad Masudi amefariki dunia kabla ya kufikishwa hospitali kwa ajili ya kupatiwa matibabu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments