WAFICHA MAITI NA KUJIZUIA KULIA KUKWEPA GHARAMA ZA KWENDA MOCHWARI



Miguu

Wananchi wa Kijiji na Kata ya Lupanga, wilaya ya Ludewa mkoani Njombe, wamesema wamekuwa wakilazimika kuficha maiti, kuzuia matangazo na kujizuia kulia unapotokea msiba jioni au mchana majumbani mwao ili kuepuka gharama za kusafirisha maiti kwenda mochwari.

Wananchi wa Kijiji hicho wameeleza changamoto hiyo katika mkutano wao na mbunge wa jimbo hilo Joseph Kamonga, alipofika katika Kijiji hicho ikiwa ni ziara yake anayoifanya katika kila Kijiji ili kupata changamoto na kuzifanyia kazi.

Zebedayo Mgaya ni mmoja wa wakazi wa Kijiji hicho aliyeeleza changamoto hiyo huku akibainisha kuwa hivi karibuni alifiwa na ndugu yake na kulazimika kukaa kimya na maiti nyumbani kwake akihofia kutangaza kwa kuwa uongozi wa Kijiji hicho ungemtaka kufikisha mwili wa marehemu mochwari iliyopo umbali wa zaidi ya Km 10 kutoka kwenye kijiji hicho huku gharama za usafirishaji pekee zikiwa ni shilingi 40,000 hadi 50,000.

"Gharama za kusafirisha mwili kutoka hapa mpaka mochwari iliyopo Mlangali ni zaidi ya Km 10 na gharama zake ni 50,000 na sijui kwanini gharama ya kusafirisha maiti ni kubwa kuliko kusafirisha mahindi, nashauri kama Mochwari ni mradi mzuri kwa Wizara ya Afya au Halmashauri basi wajenge kila kijiji mahali ambapo mtu anaweza kufikisha maiti na kurudisha nyumbani, "amesema Zebedayo Mgaya.

Aidha, wananchi wa kijiji hicho wamesema wamekuwa na hofu wanapopata msiba na kutoa taarifa kwa uongozi wa kijiji kwa kuwa imekuwa ikiwalazimu kufikisha maiti katika mochwari kutokana na kutoruhusiwa kulala na maiti huku wengi wao wakiwa hawana ada ya mochwari kwa wakati huo.

Kwa upande wake Katibu wa Chama Cha Mapinduzi wilaya ya Ludewa Baraka Mfaume, aliyeongozana na mbunge katika mkutano huo amesema chama kimepokea changamoto hiyo na kuelekeza ofisi ya mkuu wa wilaya kuifanyia.

CHANZO - EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments