UVCCM YAMVAA GWAJIMA KUHUSU CHANJO YA CORONA,YAMWITA MTOVU WA NIDHAMU

Katibu Mkuu UVCCM Kenani Kihongosi 

Na Dotto Kwilasa, Dodoma
Siku chache baada ya Mbunge wa Kawe Askofu Josephat Gwajima kutuma meseji kwa jamii Kupitia mahubiri yake akidai chanjo ya ugonjwa wa Corona haifai na huenda ikawa na madhara kutokana na alichoeleza kwamba bado haijafanyiwa utafiti wa kutosha,Jumuiya ya Umoja  wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM)imeibuka na kulaani kitendo hicho huku ikiuomba Uongozi wa Chama hicho kumchukulia hatua za kinidhamu.

Katibu Mkuu UVCCM Kenani Kihongosi amesema maneno ya Askofu huyo wa Kanisa la Ufufuo na Uzima yanagawa wananchi na kwamba ni utovu wa nidhamu kwani CCM ina taratibu zake katika kutolea maamuzi ya hoja za wananchama wake.

Akiongea na Waandishi wa habari Jijini hapa Mara baada ya kumalizika kwa  majadiliano mbalimbali ya Sekretarieti ya Jumuiya hiyo  yaliyolenga kuimarisha umoja huo,Kihongosi amesema wao Kama wanachama wa CCM wamekerwa na kauli hiyo inayoleta ukakasi  na kulenga kuigawa jamii.

"Mtu unatoka huko na kuanza kutoa kauli za kichochezi zinazowachanganya watu,kwanza sote tunafahamu kwamba yeye sio Daktari hayo maneno anayoyazungumza anauhakika gani kama chanjo hiyo ina madhara na amejuaje kama haikufanyiwa utafiti,"amesema.

Katibu huyo ameeleza kuwa Serikali Kupitia Wizara ya Afya imeshatoa maelekezo yote kuhusu chanjo hiyo na kwamba wizara hiyo inaendelea kutekeleza majukumu yake ikiwa ni Pamoja na kuhamasisha jamii kujikinga na ugonjwa huo huku wakiamini mwenye mamlaka ya Kutoa uhai kwa binadamu ni Mungu pekee.

"Amewakosea sana watanzania, Serikali ina miongozo yake na tayari inafahamika kwamba chanjo ya Corona itatolewa kwa hiari na sio lazima,kwa hiyo mtu anaweza kuchagua achanje au asichanje na sio kuchaguliwa maamuzi na isitokee mtu wa kuwapotosha watu,"amesisitiza Katibu Kihongosi.

Kuhusu msimamo wao kwa chanjo hiyo,UVCCM wamesema kuwa  wao wataendelea kusisimama bega kwa bega na Rais Samia Suluhu Hasan na kuhakikisha zoezi hilo linafanikiwa kama matarajio ya wengi yalivyo.

"Rais wetu sio Muuaji, hawezi kuingiza taifa kwenye vitu visivyofaa,sisi kwa umoja wetu hatuwezi kumuangusha tutashirikiana kwa kila kitu kuhakikisha tunasukuma gurudumu la maendeleo mbele zaidi,"amesema.

Kutokana na hayo Katibu huyo wa Jumuiya ya Vijana CCM ametumia nafasi hiyo pia kuwataka Viongozi wa dini kujielekeza katika utamaduni wao wa  kuhubiri amani na ushirikiano badala ya kujiingiza katika siasa chafu.

Amesema Viongozi hao Wana dhamana kubwa ya maisha ya watu hivyo ni wakati wa kujikita kushughulika na masuala yanayowahusu 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments