DKT. NCHEMBA AAGIZA FEDHA ZA MAENDELEO ZIPEWE KIPAUMBELE KWENYE UTEKELEZAJI WA BAJETI


 Na. Josephine Majura, WFM, Dodoma
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), amewaagiza watendaji wa Wizara hiyo kuhakikisha kuwa hakuna Wizara ama taasisi itakayopelekewa chini ya asilimia 50 ya bajeti yake ya maendeleo katika bajeti ya Serikali iliyooanza kutelezwa kuanzia Julai mosi mwaka huu.

Ametoa Maagizo hayo wakati akizungumza na watumishi wa Wizara hiyo katika ukumbi wa mikutano wa  Mwalimu Nyerere wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP),  jijini Dodoma ambapo pamoja na mambo mengine ametoa mwelekeo wa utekelezaji wa Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2021/2022.

“Nataka mkasimaie ugawaji wa rasilimaji fedha kwa kila Wizara ili tukirudi tena bungeni kuelezea utekelezaji wa bajeti kusiwe na mahali ambapo fedha za maendeleo zitakuwa zimepelekwa chini ya asilimia 50” Alisisitiza Dkt. Nchemba.

Aidha, aliwaagiza watumishi hao kujiwekea utaratibu wa kufuatilia kwa umakini utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo inayotokana na fedha zinakazotolewa na Serikali ili kuona utekelezaji wake na kama zimetumika kama ilivyokusudiwa kwa kuwa itasaidia miradi kukamilika kwa wakati.

Aidha, aliwataka watumishi hao kuendelea kufanya kazi kwa weledi mkubwa kwa kuzingatia maadili, kanuni na taratibu za Utumishi wa Umma.

Dkt. Mwigulu aliongeza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano Mhe. Samia Suluhu Hassan anaitegemea wizara katika masuala yote ya uchumi hivyo ni jukumu la Wizara kuhakikisha inatoa ushauri mbalimbali wa kitaalamu kuhusu masuala ya uchumi kwa maendeleo ya nchi.

Vile vile Dkt. Mwigulu aliwataka watumishi hao kuwa wabunifu hususan katika kubuni vyanzo vipya vya mapato ili kuisaidia Serikali katika kukuza uchumi wa nchi.

Alitoa wito kwa watumishi kuendelea kutumia fursa za mafunzo zilizopo ili kujiongezea ujuzi, lakini pia aliagiza kuwepo na utaratibu mzuri ambao kila mtumishi atapata nafasi ya kuhudhuria mafunzo ya muda mrefu na muda mfupi ili kuongeza ujuzi kwenye taaluma zao.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, aliwapongeza watumishi kwa ufanyaji kazi na kuwataka waendelee kufanya kazi kwa weledi ili kuhakikisha jukumu la kusimamia uchumi wa nchi inatekelezwa kwa ufanisi zaidi.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali  Bw. Emmanuel Tutuba, alisema kuwa Wizara inaendelea kusimamia uchapaji kazi, maadili na maslahi ya watumishi ambapo watumishi wamepandishwa vyeo na kupandishwa madaraja.

“Tumewapandisha madaraja na kuwabadilishia miundo watumishi 529 baada ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kuelekeza watumishi wote wapandishwe madaraja wakati wa Siku ya wafanyakazi Mei Mosi na pia tumewathibitisha kazini watumishi 31” alisema Bw. Tutuba

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango anayeshughulikia Utawala Dkt. Khatibu Kazungu alimhakikisha Waziri wa Fedha na Mipango kwamba atasimamia utaribu wa mafunzo kwa watumishi ili kuwajengea uwezo katika taaluma zao na kuwaongezea ufanisi wakati wa utekelezaji wa majukumu yao.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango anayeshughulikia Uchumi Bw. Adolf Ndunguru alisema kuwa Wizara itaimarisha eneo la utafiti ili kuiwezesha Wizara kusimamia uchumi wa nchi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments