STAMIGOLD YANOGESHA MAONESHO YA BIASHARA NA TEKNOLOJIA YA MADINI SHINYANGA....YASHUKURU SERIKALI KUWAPA UMEME


Afisa Utumishi wa Kampuni ya STAMIGOLD, Muhunda Nyakiroto (kulia) akimwelezea Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya (wa pili kushoto) shughuli wanazofanya kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.

Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Kampuni ya STAMIGOLD ambayo ni kampuni tanzu ya Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) kupitia mgodi wake wa Stamigold Biharamulo (Stamigold Biharamulo Mine - SBM) uliopo wilayani Biharamulo mkoa wa Kagera umeishukuru serikali kwa kupeleka huduma ya umeme wa TANESCO hali ambayo itapunguza gharama za uendeshaji kutoka shilingi Bilioni 1.2 hadi shilingi milioni 400 au 300 kwa mwezi.

Shukrani hizo zimetolewa na Afisa Utumishi wa Kampuni ya STAMIGOLD, Muhunda Nyakiroto leo Jumapili wakati Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya akitembelea banda la Kampuni ya STAMIGOLD kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga yanayofanyika Uwanja wa Zainab Telack katika kijiji cha Butulwa kata ya Old Shinyanga Manispaa ya Shinyanga.

Afisa Utumishi wa Kampuni ya STAMIGOLD, Muhunda Nyakiroto amesema wanaishukuru serikali kwa kuwapelekea huduma ya umeme wa TANESCO kutoka Geita hali ambayo itasaidia gharama kubwa ya uzalishaji wa madini ya dhahabu ambapo wamekuwa wakitumia genereta za dizeli na sasa wataanza kupata huduma hiyo mwezi Septemba mwaka huu kwa mujibu wa TANESCO ambao sasa wanajenga kituo cha kupozea umeme.

"Tangu mgodi huu uwe chini ya Serikali mwaka 2013, na kuanza uzalishaji rasmi mwaka 2014, umekuwa ukiingia kwenye gharama kubwa ya kutumia Genereta na mafuta ya Diesel yenye gharama za Shilingi Bilioni 1.2 kwa mwezi na baada ya kupata huduma ya umeme gharama itapungua na tutatumia shilingi Milioni 300 au 400",amesema Nyakiroto.

Katika hatua nyingine, Nyakiroto amesema wanashiriki maonesho ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga kwa ajili ya kuonesha jinsi wanavyofanya shughuli za uchimbaji madini ya dhahabu pamoja kueleza manufaa ya mgodi wao kwa wananchi.

“Miongoni mwa manufaa wanayopata wananchi kupitia Mgodi wa STAMIGOLD chini ya Meneja Mkuu wa mgodi Mhandisi Gilay Shamika umetoa ajira. Mgodi umeajiri jumla ya Watanzania 610, kati ya hao 236 wameajiriwa na SBM na waliobaki  ni vibarua na wengine wameajiriwa na Wakandarasi.

 Pia tumesaidia ujenzi wa miundo mbinu na miradi kwa jamii ikiwemo ujenzi wa zahanati ya Nampalahala na ukarabati wa barabara za vijiji vya Mavota, Mkunkwa na Msalabani vilivyopo katika kata ya Kaniha wilaya ya Biharamulo Mkoani Kagera”,ameeleza Nyakiroto.

“Hali kadhalika tunatumia maonesho haya kuonesha zao jipya la mkaa mbadala unaotumia makaa ya mawe ‘Rafiki Briquate’ kutoka STAMICO ili kutunza mazingira. Bei ya mkaa huu mbadala ni rafiki lakini pia mkaa huu hautoi moshi. Tutaanza uzalishaji kamili wa mkaa mbadala mwishoni mwa mwaka huu 2021”,amesema.

Amesema Mgodi wa STAMIGOLD pia unaendelea kusaidia wajasirimali kwa kununua bidhaa zao kama vile ng’ombe kwa ajili ya nyama, mboga mboga, matunda na samaki katika masoko ya Runzewe na Chato.

Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya ameupongeza Mgodi wa STAMIGOLD kwa hatua inayoendelea nazo katika uzalishaji wa madini akieleza kuwa faida imekuwa ikipanda kila Mwaka na kusaidia STAMICO kulipa gawio Serikalini.
Afisa Utumishi wa Kampuni ya STAMIGOLD, Muhunda Nyakiroto (kulia) akimwelezea Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya (wa pili kushoto) shughuli wanazofanya kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga yanayofanyika Uwanja wa Zainab Telack katika kijiji cha Butulwa kata ya Old Shinyanga Manispaa ya Shinyanga. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Afisa Utumishi wa Kampuni ya STAMIGOLD, Muhunda Nyakiroto (kulia) akimwelezea Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya (wa pili kushoto) shughuli wanazofanya kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga
Afisa Utumishi wa Kampuni ya STAMIGOLD, Muhunda Nyakiroto (kulia) akimwelezea Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya (katikati) shughuli zinazofanywa na kampuni hiyo kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga
Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya(katikati) akiangalia vipeperushi na bidhaa mbalimbali kwenye banda la Kampuni ya STAMIGOLD katika Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya(katikati) akiondoka kwenye banda la Kampuni ya STAMIGOLD katika Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya(kushoto) akiondoka kwenye banda la Kampuni ya STAMIGOLD katika Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.

Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments