BENKI YA CRDB YAZINDUA MSIMU WA PILI WA KAMPENI YA 'MTAANI KWAKO' KAHAMA


Meneja wa Benki ya CRDB kanda ya magharibi Said Pamui na mwakilishi wa mkuu wa wilaya ya Kahama Robert Kwela wakinyanyua bendera ikiwa ni ishara ya uzinduzi rasmi wa msimu wa pili wa kampeni ya mtaani kwako.

Na Salvatory Ntandu - Kahama

Benki ya CRDB imezindua msimu wa pili wa kampeni ya mtaani kwako ambayo inalenga kuwaunganisha wafanyabiashara wakubwa na wa kati wakiwemo wajasiriamali, waendesha bodaboda, mamalishe na huduma bunifu zinazotolewa na benki hiyo ili kuboresha Maisha yao katika nyanya mbalimbali za kiuchumi.

Kampeni hiyo imezinduliwa leo katika manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga na mwakilishi wa mkuu wa wilaya ya Kahama, Robert Kwela ambapo amesema kuwa serikali itaiunga mkono benki hiyo katika huduma mbalimbali za kifedha wanazotaka kuzipeleka kwa wananchi hususani wajasiriamali wadogo.

Alisema kuwa kampeni hiyo imebeba maudhui ya kuielimisha jamii kuhusiana na umuhimu wa kutunza fedha,kuchangamkia fursa zinazotolewa na taasisi za kifedha kama vile mikopo na bima mbalimbali katika biashara zao au vyombo vya usafiri wanazovimiliki.

“Kampeni hii ijikite kutoa elimu kwa jamii ili itambue umuhimu wa kutunza fedha benki na mtoe elimu ya utunzaji wa fedha kwa wajasiriamali wadogo kabla ya kuwapatia mikopo ili waendelee kufurahia huduma mnazowapatia ikiwemo huduma za kifedha kupitia simu za mkono,”alisema Kwela.

Sambamba na hilo Kwela ameishauri benki ya CRDB kuwashirikisha wenyeviti wa vijiji na mitaa ili kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma hiyo ya kufunguliwa akaunti zisizokuwa na makato kila mwezi ili waweze kukuza vipato vyao na kuachana na tabia ya kuweka fedha majumbani.

Awali akimkaribisha mgeni rasimi meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi Said Pamui amesema kuwa kampeni hiyo itawaunganisha wananchi na huduma mbalimbali zinazotolewa na benki hiyo ikiwa ni pamoja na kupata akaunti isiyokuwa na makato,bima za biashara,mikopo yenye riba nafuu itakayoweza kuweza kuwasaidia kukuza mitaji yao.

Alisema kuwa kwa kutambua umuhimu na mchango wa kundi la wajasiriamali katika ujenzi wa uchumi CRDB imewaletea huduma maalumu ya “Hodari” akaunti maalumu isiyokuwa na makato pindi unapoweka au kutoa fedha katika ATM na mawakala wa benki hiyo.

“Hodari ni huduma maalumu kwa wajasiriamali nitoe fursa kwao kuichangamkia fursa hii wakiwemo,mamalishe,wauza magenge,wenye maduka ya rejareja,na wamachinga,ambao sisi CRDB tumeona tuwasidie ili waweze kukuza mitaji yao,”alisema Pamui.

Hata hiyo Pamui amesema kuwa kampeni hiyo imerudiwa kutokana na kupokea maombi kutoka kwa wateja wao wakitaka irudiwe ambapo kwa mwaka huu CRDB imejipanga kuwafuata wateja wake popote walipo na kuwapa elimu ya fedha.

“Tutahamasisha matumizi ya njia mbadala za utoaji huduma za fedha kwa njia za mawakala,Simubanking,internate banking na matumizi ya akauti za Tembo Card na umuhimu wa bima.

Musa Juma ni mwendesha bodaboda ambaye amepata fursa ya kupatiwa elimu kuhusiana na kampeni ya mtaani kwako iliyotolewa na maafisa wa CRDB amesema kuwa itamsaidia kutunza fedha kwa urahisi na kuacha na tabia ya kutunza fedha nyumbani ambapo muda mwingi hupotea kutokana na kukosa usalama.

“Binafsi nilikuwa natunza fedha kwenye kibubu ambacho huwa nakiweka chini ya kitanda changu lakini usalama wa fedha maranyingi huwa ni mdogo kwani mwaka 2017 niliibiwa kibubu changu na kupata hasara ya zaidi ya shilingi laki tano,”alisema Juma.
Kushoto ni Meneja wa Benki ya CRDB kanda ya magharibi Said Pamui na mwakilishi wa mkuu wa wilaya ya Kahama Robert Kwela wakinyanyua bendera ikiwa ni ishara ya uzinduzi rasmi wa msimu wa pili wa kampeni ya mtaani kwako.
Mwakilishi wa mkuu wa wilaya ya Kahama ,Robert Kwela akizungumza na wananchi na wajasiriamali mbalimbali waliohudhuria uzinduzi wa kampeni ya mtaani kwako katika viwanja vya National Housing katika manispaa ya Kahama.
Meneja wa Benki ya CRDB kanda ya magharibi Said Pamui akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni ya mtaani kwako katika viwanja vya National Housing katika manispaa ya Kahama.
Meneja wa Benki ya CRDB kanda ya magharibi Said Pamui akitoa elimu kuhusu umuhimu wa bima kwa waendesha pikipiki waliohudhuria uzinduzi wa kampeni ya mtaani kwako katika manispaa ya Kahama.
Askari polisi wa kikosi cha Usalama barabarani wilaya ya Kahama akikagua leseni ya Meneja wa Benki ya CRDB kanda ya magharibi wa CRDB Said Pamui kabla ya msafara wa waendesha pikipiki wa manispaa ya Kahama kuanza maandamano ya kuelekea katika eneo la uzinduzi wa msimu wa pili wa kampeni ya mtaani kwako.
Meneja wa mawasiliano wa benki ya CRDB, Paschal Chuwa akitoa elimu kuhusiu umuhimu wa bima kwa waendesha bodaboda wa manispaa ya Kahama kabla ya kuanza maandamano ya kuelekea katika eneo la uzinduzi wa msimu wa pili wa kampeni ya mtaani kwako.


Vikundi mbalimbali vikitoa burudani kwa wananchi waliohuduria uzinduzi wa msimu wa pili wa kampeni ya mtaani kwako.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments