RC MAKALLA ATANGAZA KIAMA KWA WEZI WA MAFUTA KIGAMBONI


Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Amos Makalla ametangaza Vita na Mtandao wa wezi wa mafuta ghafi kupitia bomba kuu la mafuta Kigamboni na kulielekeza Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es salaam kuwashughulikia kikamilifu wezi hao ambapo hadi leo jumla ya watuhumiwa 15 wanashikiliwa.

RC Makalla amesema hayo leo wakati wa ziara ya kukagua miundombinu ya kupokea mafuta ghafi kutoka kwenye Meli za Mafuta hadi kwenye Visima ambapo ameshuhudia uharibifu mkubwa wa miundombinu uliofanywa na Mkazi mmoja aliyechimba handaki hadi kwenye Bomba kuu la mafuta na kujiunganishia jambo lililopelekea hasara ya upotevu wa mafuta kwa wafanyabiashara.

Aidha RC Makalla amejionea namna mkazi huyo alivyokuwa akiyapakia mafuta hayo ya wizi kwenye Magari makubwa ya kubeba kokoto na mchanga ambayo ndani yake yamefungwa matanki makubwa ya mafuta na juu zinapangwa kokoto ili kuwazuga watu.

Kutokana na wizi huo RC Makalla ameeleza kutoridhishwa na maelezo aliyopewa na TPA na Wakala wa uagizaji Mafuta kwa pamoja na kuamua  kuitisha kikao cha pamoja siku ya Jumatatu kwenye ukumbi wa Anatoglo kitakachojumuisha Waagizaji Mafuta, TPA, TRA na Wadau wote wa mafuta ili wajadili namna bora ya kuhakikisha tatizo hilo halijirudii na kupitia mikataba yao hususani kipengele cha namna gani mfanyabiashara aliyepokea Mafuta pungufu tofauti na yale aliyolipia anafidiwa.

Wakati huo huo RC Makalla amefanya kikao cha pamoja na Baraza la Madiwani na Watendaji Wilaya ya Kigamboni ambapo amewapatia vipaumbele ikiwemo utatuzi wa kero za wananchi, suala la usafi, ukusanyaji wa Mapato, usimamizi wa miradi ya maendeleo, ulinzi na usalama na mambo mengine.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments