NAIBU WAZIRI MAMBO YA NDANI YA NCHI AWAJULIA HALI MAJERUHI BASI LA CLASSIC, DEREVA ADAKWA

 Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Khamis Hamza Chilo akizungumza na waandishi wa Habari ,alipotembelea kuona majeruhi wa ajali ya basi katika Hospitali ya Rufaa mkoa wa Shinyanga

****

Na Marco Maduhu, Shinyanga

NAIBU Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Khamis Hamza Chilo, amesikitishwa na ajali ya basi la Classic iliyotokea jana mkoani Shinyanga, na kuonya madereva wa vyombo vya moto kuacha kuendesha mwendo kasi ili kuepuka ajali zisizo za lazima.

Amebainisha hayo leo wakati akizungumza na waandishi wa habari, alipotembelea majeruhi wa ajali hiyo katika Hospitali ya Rufaa mkoa wa Shinyanga.


Amesema madereva wa vyombo vya moto wanapaswa muda wote kuzingatia sheria za usalama barabarani, hasa pale wanapokuwa na abiria, ili kutosababisha ajali ambazo hugharimu maisha ya watu.

“Katika ajali hii ya basi hapa mkoani Shinyanga, nimeambiwa chanzo chake ni mwendokasi hivyo nawaomba madereva wazitii sheria za usalama barabarani ili kuepuka ajali zisizo za lazima na kugharimu maisha ya watu,”amesema Chilo


Naye Kaimu Mganga mfawidhi wa hospitali ya Rufaa mkoani Shinyanga Dkt. Agostine Maufi, amesema katika majeruhi 26 waliowapokea jana, Sita wamepewa Rufaa ya kwenda kutibiwa Bugando Jijini Mwanza, na 20 waliobaki wanaendelea na matibabu na hali zao ni nzuri.

Kwa upande wake Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Shinyanga ACP Debora Magiligimba, amesema Jeshi hilo limefanikiwa kumkamata Dereva wa basi hilo Maxison Mkuru, ambaye alikimbia mara baada ya kutokea ajali, ambapo wanamhoji na atachukuliwa hatua kali za kisheria.


Aidha katika ajali hiyo ya basi ambayo ilitokea jana katika jijiji cha Buyubi kona ya Didia wilayani Shinyanga, na basi la Kampuni ya Classic likitokea Kampala nchini Uganda kwenda Jijini Dar es salaam lilisababisha vifo vya watu wanne na kujeruhi watu zaidi ya 20.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments