VIJANA 48,000 KUNUFAIKA NA MAFUNZO YA USAFI WA MWILI NA MAZINGIRA YANAYOTOLEWA NA RALEIGH TANZANIA

 

Baadhi ya Vijana wa shirika lisilo la kiserikali la Raleigh Tanzania, kupitia Mradi wa Vijana na Mabadiliko Chanya wakifanya Usafi katika Soko la Mavunde Chang’ombe leo April 15,2021 jijini Dodoma.


     


Vijana wa shirika lisilo la kiserikali la Raleigh Tanzania, kupitia Mradi wa Vijana na Mabadiliko Chanya wakikabidhi Vifaa vya Kutunzia Taka katika Soko la Mavunde Chang’ombe leo April 15,2021 jijini Dodoma.

Baadhi ya Vijana wa shirika lisilo la kiserikali la Raleigh Tanzania, kupitia Mradi wa Vijana na Mabadiliko Chanya wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kumaliza kufanya Usafi katika Soko la Mavunde Chang’ombe leo April 15,2021 jijini Dodoma.

Baadhi ya Wanafunzi wa Sekondari ya Dodoma wakipata elimu ya usafi kutoka katika shirika lisilo la kiserikali la Raleigh Tanzania, kupitia Mradi wa Vijana na Mabadiliko Chanya leo April 15,2021 jijini Dodoma.

Mratibu wa Mradi “Vijana na mabadiliko chanya kitabia juu ya usafi” kutoka Shirika lisilo la Kiserikali la Raleigh Tanzania Augusto Dickson,akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kufanya usafi katika soko la Mavunde Chang’ombe pamoja na kutoa elimu kwa Wanafunzi wa shule ya Sekondari Dodoma Leo April 15,2021 jijini Dodoma

Mmoja wa vijana wanufaika wa mafunzo hayo Dorice Kimambo,akielezea jinsi walivyofaindika na elimu kuhusu Usafi wa Mwili na Mazingira.

Muhamasishaji wa Masuala ya Usafi Bw.Issa Mohamed,akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kufanya usafi katika soko la Mavunde Chang’ombe pamoja na kutoa elimu kwa Wanafunzi wa shule ya Sekondari Dodoma Leo April 15,2021 jijini Dodoma


Na.Alex Sonna,Dodoma

Vijana 48,000 katika Mikoa Minne wanatarajia kupata elimu ya utunzaji wa mazingira na usafi wa Mwili kupitia shirika Lisilo la Kiserikali la Raleigh Tanzania wanaoendesha mradi wa “Vijana na mabadiliko chanya kitabia juu ya usafi” ili kubadilisha tabia na kuepuka Magonjwa Mbalimbali.

Hayo yamesemwa Leo April 15,2021 na Mratibu wa mradi huo Augostino Dickson, wakati akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya vijana walio katika maradi huo kufanya usafi katika soko la Mavunde Chang’ombe pamoja na kutoa semina kwa Wanafunzi wa shule ya Sekondari Dodoma.

Bw.Dickson amesema kuwa mradi huo hivi sasa unatekelezwa katika mikoa ya Dar es saalam, Dodoma, Morogoro pamoja na Iringa.

Amesema kuwa mradi huo umelenga katika kubadilisha mitazamo ya vijana katika masuala ya usafi ambayo yamekuwa hayapewi kipaumbele hali inayosababisha uchafu kuzagaa katika maeneo mengi.

“Mradi wetu umelenga kuleta mabadiliko chanya kitabia kwa vijana na unahusisha vijana kutoa mafunzo kwa vijana wenzao ili kupanua wigo wa uelewa juu ya usafi na mazingira”amesema Dickson.

Aidha amesema kuwa kupitia mradi huo walifanya tafiti kuona ni jinsi gani wanaweza kuendesha mafunzo ya usafi kwa vijana ili kuwabadili mitazamo yao.

“Vijana ndiyo kundi kubwa katika taifa hivyo tuliona kuwa kwa kuwataumia wao tutaweza kubadili mitazamo iliyopo katika jamii na kuleta mabadiliko chanya katika suala la usafi”amesisitiza

Hata hivyo amesema kuwa pamoja na kutoa mafunzo haya lakini pia wamekuwa wakishirikiana katika kufanya usafi katika maeneo mbalimbali na kutoa msaada wa vifaa vya kufanyia uasafi na kuhifadhia taka katika maeneo kama walivyofanya ambavyo leo katika soko la Mavunde Chang’ombe na shule ya sekondari ya Dodoma.

Kwa upande wake Afisa afya jiji la Dodoma Abdallah Mahia amesema, kutoa elimu katika shule kutasaidia wa wanafunzi kukua katika mazingira ya kutambua umuhimu wa usafi ili kupepukana na magonjwa ya mlipuko.

"Sisi kama serikali Kwa kushirikiana na Wizaraya Afya na Tamisemi, tunaungana nanyi katika kuhamasisha uelewa wa kufanya usafi na kutunza mazingira"amesema Mahia.

Naye Mmoja wa vijana wanufaika wa mafunzo hayo Dorice Kimambo, amesema kuwa wamejifunza mambo mbalimbali yanayohusu usafi na baadaye wanaenda katika jamii kutoa elimu na kusaidia kubadili mitazamo iliyopo juu ya usafi.

“Katika maeneo tunayokwenda kutoa elimu tumebaini bado zipo changamoto kadhaa ikiwemo watu kuishi kwa mazoea imekuwa kikwazo kupata mabadiliko kwa haraka, watu wengi wanadai kuwa hawana fedha za kununulia vifaa vya kuhifadhia taka au kulipia magari ya kubeba taka”amesema Kimambo

Shirika la Raleigh Tanzania limeendesha Zoezi la Usafi Katika Soko la Mavunde la Chang'ombe pamoja na kutoa elimu katika Shule ya Sekondari Dodoma ikiwa ni katika kuadhimisha kilele cha mradi huo ulioratibiwa miezi miwili iliyopita.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments