KAIMU AFISA VIJANA MKOA WA SINGIDA FREDERICK NDAHANI AISHAURI SERIKALI KUFUFUA SHULE ZA UFUNDI

 

Kaimu Afisa Vijana Mkoa wa Singida, Frederick Ndahani (wa pili kushoto) akizungumza na Walimu wa Ufundi  wa Shule ya Msingi Makiungua iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi mkoani Singida alipoitembelea juzi kwa lengo la kukagua uwezeshwaji mafunzo na ujuzi kwa vijana.

Madawati yakitengenezwa. na Shule ya Msingi Makiungu iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi mkoani Singida.
Madawati yaliyotengenezwa.
Kaimu Afisa Vijana Mkoa wa Singida, Frederick Ndahani (kulia) akikagua utengenezaji wa madawati.
Madawati yaliyotengenezwa.

Na Dotto Mwaibale, Singida.

KAIMU Afisa Vijana mkoani hapa,  Frederick Ndahani ameishauri Serikali kufufua Shule za Msingi za ufundi Nchini. 

Ndahani alitoa ushauri huo juzi alipotembelea  Shule ya Msingi Makiungu iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi mkoani Singida kwa lengo la kukagua uwezeshwaji mafunzo na ujuzi kwa vijana.

Ndahani alisema Shule ya Msingi Makiungu ni moja ya shule zilizofanya  vizuri katika mradi waliopewa wa kutengeneza madawati 1000  ya shule za msingi zilizopo wilayani humo.

Ndahani alisema shule hiyo ya mchepuo wa ufundi   ni moja ya shule inayoifanya vizuri na kusababisha ofisi ya mkurugenzi wa wilaya ya  Ikungi kuwapa kazi ya kutengeneza madawati hayo.

" Shule hizi za mchepuo wa ufundi hapa nchini zikiboreshwa zinaweza kusawaidia vijana wa kitanzania kupata ujuzi wa ufundi mbalimbali." alisema Ndahani.

Alisema  wanafunzi wanaojiunga katika shule hiyo hapa ni wale ambao wamekosa nafasi ya kuendelea na elimu ya sekondari na vyuo na kuwa faida wanayoipata ni kupata mafunzo hayo ya ufundi bure  kama ilivyo elimu ya msingi.

Alisema  kuboreshwa kwa shule  hizo kutasaidia kupata mafundi ambao watatumika kukarabati samani mbalimbali zilizopo mashuleni badala ya kuwapa mafundi kutoka nje ambao watahitaji kulipwa fedha nyingi.

Kwa upande wao  Walimu wa Ufundi katika shule hiyo Cosmas Uhiku na  Haji Kidabu Wameiomba Serikali kuwapatia vifaa vya kutosha kwani wanao uwezo wa kuwapatia vijana mafunzo ya kisasa  sanjari na vyeti baada ya kumaliza mafunzo kwa muda wa miaka miwili.

Mwalimu mkuu wa shule hiyo  Hashimu Ntandu amemshukuru Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, Justice Kijazi kwa kuwapatia mradi huo mkubwa wa kutengeneza madawati ambapo wanatengeneza kwa gharama nafuu.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments