BENKI YA EXIM YAMWAGA ZAWADI ADA ZA SHULE, SAFARI ZA SERENGETI KWA WASHINDI WA CHANJA KIJANJA

Mkuu wa Idara ya Kidigitali na Huduma Mbadala wa benki ya Exim Bw Silas Matoi (Katikati) akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa hafla ya kutangaza washindi wa kampeni ya benki hiyo ijulikanayo kwa jina la ya 'Chanja Kijanja na Exim Mastercard' iliyolenga kuhamasisha wateja wa benki hiyo kutumia kadi katika manunuzi ya mtandaoni au kufanya malipo kupitia mashine za malipo (POS). Wengine ni pamoja na Maofisa waandamizi wa benki hiyo Bw Callist Butinga (Kushoto) na Paritosh Babla.

Na Mwandishi wetu - Dar es salaam
Benki ya Exim hii leo imetangaza washindi wa kampeni yake ya 'Chanja Kijanja na Exim Bank Mastercard', huku ikigawa zawadi mbalimbali kwa washindi hao ikiwemo ada za shule pamoja na safari ya kutembelea hifadhi ya Serengeti kwa washindi wa jumla wa kampeni hiyo.

Kampeni hiyo iliyodumu kwa mwezi mmoja, ilianza Desemba mwaka jana, ikilenga kuhamasisha wateja wake kutumia kadi za MasterCard za benki hiyo wanapofanya manunuzi au malipo ya mahitaji muhimu kwenye maduka (Shopping) pamoja na ununuzi wa bidhaa kimataifa kupitia mtandaoni.

Kati ya washindi watatu wa jumla wa kampeni hiyo, ilishuhudiwa washindi wawili wakichagua zawadi ya kulipwa ada ya shule pamoja na vifaa vyote vya shule kwa mtoto mmoja kwa kila mshindi, wakati mshindi mmoja akichagua zawadi safari ya kutembelea Hifadhi ya Taifa Serengeti akiwa na mwenza wake huku kila kitu kikiwa kimelipiwa. 

“Benki ya Exim inaelewa changamoto ambazo wazazi wanakabiliwa nazo wakati wa kufungua shule. Wafanyakazi wetu wengi ni wazazi pia, kwa hivyo tunaelewa hizi changamoto. Tunaamini zawadi za namna hii zitapunguza mzigo wa kifedha kwa wazazi na walezi katika katika kipindi hiki. "alisema Mkuu wa Idara ya Kidigitali na Huduma Mbadala wa benki hiyo Bw Silas Matoi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kwenye hafla hiyo iliyofanyika makao makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam.

Alisema kampeni hiyo imehitimishwa kwa mafanikio makubwa yaliyotokana na muitikio mkubwa kutoka kwa wateja wa benki hiyo hatua ambayo inadhihirisha uhalisia wa huduma zinatolewa na benki hiyo kwa wateja wa benki hiyo.

"Kwa muitikio huu tumebaini ongezeko kubwa la matumizi ya huduma zetu za kidigitali kutokana mwenendo wa mfumo wa maisha wa wateja wetu kitu kinachotupa mrejesho muhimu utakaotusaidia kuendelea kubuni huduma bora zaidi zinazoendana na hitaji hilo la wateja wetu. Zaidi tunashukuru na kujivunia zaidi kuona kwamba wateja wetu wanafurahia huduma zetu kulingana na matarajio yao ambayo ni kupata huduma za haraka, rahisi na salama kwao,’’ aliongeza.

Zaidi Bw. Matoi alihamasisha wateja wa benki hiyo kuendelea kufurahia huduma za kidigitali hata baada ya kuisha kwa kampeni hiyo.

Kwa upande wao washindi Baraka Kimaro, Khamis Mansour na Mustafa Albaghdadi wote walionyesha furaha yao na shukrani baada ya kupokea habari za ushindi huo huku wakielezea kuridhishwa zaidi na uhakika na ubora wa huduma za kibenki ikiwemo zile za mtandaoni na kwenye matawi wanazopata kupitia taasisi hiyo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments