WAZIRI BITEKO : UCHIMBAJI WA MAKAA YA MAWE KWENYE MRADI WA STAMICO LAZIMA UANZE


Na Mathias Canal, Wazo Huru-Dodoma
Serikali imeeleza dhamira yake ya kuanza uchimbaji wa makaa ya mawe kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO).

Waziri wa Madini Mhe Doto Biteko ameeleza mpango huo wa serikali wakati akizungumza kwenye kikao kazi na watumishi wote wa Wizara hiyo kilichofanyika katika Mji wa serikali Mtumba Jijini Dodoma tarehe 11 Disemba 2020.

Katika kikao kazi hicho kilichochagizwa na mapokezi ya Naibu Waziri wa Madini Mhe Prof Shukrani Manya, Waziri Biteko amebainisha kuwa changamoto na mvutano uliopo baina ya Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) unapaswa kufika ukomo ili shughuli za uchimbaji makaa ya mawe uweze kusonga mbele.

Amesema kuwa viongozi wote wa Wizara ya Madini wanapaswa kushirikiana kwa pamoja ili kufanikisha dhamira hiyo ya serikali kwa maslahi makubwa na manufaa ya wananchi.

“Tutakuwa na urafiki mahali tutakapokuwa tunafanya vizuri na kununiana pale ambapo hatutafanya vizuri na mimi kiu yangu ni kuona wote tunafanikiwa” Amesema Biteko

Awali Waziri Biteko amewaasa watendaji wa Wizara hiyo ya Madini kubadilika kutokana na mazingira kwani mazoea waliyokuwa nayo kabla ya uteuzi wa Naibu Waziri yanapaswa kumalizika na kulinda heshima ya viongozi hao.

“Mazoea sio mahala pake kwa sasa, na mkiona Mhe Rais amemteua kiongozi kutoka kwenye Wizara ya Madini maana yake ameona utendaji uliotukaka kwani ana watanzania wengi wenye uwezo wa kufanya kazi kwa weledi lakini wakati mwingine anatoa upendeleo” Amekaririwa Mhe Biteko

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Madini Mhe Prof Shukrani Manya amesema kuwa matokeo mazuri ya ufanyaji kazi wa watendaji wa Wizara ya Madini ndio umempatia ngazi ya kupanda daraja hivyo amewataka kuongeza bidii na ufanisi katika kazi ili kufikia adhma ya serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Mhe Rais Dkt John Pombe Magufuli.

Mhe Manya amewasisitiza watumishi wote kuendeleza ushirikiano ili kufikia dhamira ya ilani ya uchaguzi ya CCM 2020/2025 pamoja na mikakati madhubuti ambayo wizara na taasisi zake imejiwekea.

MWISHO


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments