RAIS MAGUFULI AWATAKA WATANZANIA KUENDELEA KUMSHUKURU MUNGU..ATEMBEZA KAPU KANISANI

 Rais wa Tanzania, Mhe. Dkt.John Pombe Magufuli leo Disemba 25, 2020 ameungana na Waumini wa Kanisa Katoliki Parokia ya Bikira Maria Imakulata, Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma kusali Misa Takatifu ya Krismasi ambayo ni maadhimisho ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo.






Rais Dkt. John Magufuli, akipitisha kapu la sadaka kwa waumini wakati wa ibada Takatifu ya Sikukuu ya Christmas

Katika ibada hiyo Rais Dkt. Magufuli pia amepitisha kapu la sadaka kwa waumini wa kanisa hilo.

Baada ya Misa hiyo iliyoongozwa na Paroko wa Parokia hiyo Padre Paul Mapalala, Mhe. Rais Magufuli amewapongeza na kuwatakia heri Watanzania wote kwa sikukuu ya Krismasi na amewataka kuendelea kumshukuru Mungu kwa miujiza na upendo mkubwa anaolitendea Taifa la Tanzania.

Mhe. Rais Magufuli amesema upendo na miujiza ya Mungu kwa Tanzania inajidhihirisha katika kipindi hiki ambapo dunia inapita katika wakati mgumu wa janga la ugonjwa wa Corona (Covid-19) ambapo maelfu ya watu wanaendelea kupoteza maisha kila siku, lakini Tanzania imeepushwa na janga hilo na maisha ya Watanzania yanaendelea kama kawaida.

Amewaomba Watanzania wote waendelee kumshukuru na kumuomba Mungu aendelee kulilinda Taifa lao dhidi ya ugonjwa huo, na kuwaombea wananchi wa Mataifa mengine waepushwe na Corona.

Ametoa wito kwa viongozi wa Mataifa mbalimbali duniani kukubali kumuweka Mungu mbele katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Corona badala ya kutegemea nguvu za binadamu pekee.

Pamoja na kuwatakia heri ya Krismasi, Mhe.Rais Magufuli amewataka Watanzania kuendelea kuchapa kazi za uzalishaji mali ili kuendelea kujenga Taifa lao pamoja na kuhakikisha wanamtanguliza Mungu kwa kila jambo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments