VETA, WADAU WAWEKA MIKAKATI UZALISHAJI WA WATAALAMU MAHIRI WA SEKTA ZA KILIMO, UKARIMU NA UTALII


Mkurugenzi Mkuu wa VETA Dkt. Pancras Bujulu akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha kati ya VETA na wadau wa sekta za Kilimo, Ukarimu na Utalii wanaotekeleza programu ya Uanagenzi Pacha (Dual Apprenticeship Training System) iliyofanyika mkoani Manyara tarehe 30 Desemba, 2020.
Balozi wa programu ya Uwanagenzi Pacha na Mkulima wa mjini Babati, Ndugu Jitu Son, akichangia mada wakati wa warsha hiyo. 
Washiriki wa warsha wakiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa VETA Dkt. Pancras Bujulu (katikati). Kulia kwake ni Mkurugenzi wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi Bi. Stella Ndimubenya na Mkuu wa Chuo cha VETA Manyara Ndugu Felix Ole Ndukai. Kushoto kwake ni Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Kati Ndugu John Mwanja na Balozi wa programu ya Uanagenzi Pacha na Mkulima wa mjini Babati Ndugu Jitu Son.
Mratibu wa Programu ya Uwanagenzi Pacha VETA, Ndugu Francis Komba, akisisitiza jambo kwa washiriki wakati akiwasilisha mada juu ya wajibu wa wadau hao katika kufanikisha utoaji mafunzo kwenye sekta hizo.
Mmoja wa washiriki akichangia mada wakati wa warsha hiyo.
Washiriki wa warsha hiyo walipotembelea moja ya karakana inayotumika kutoa mafunzo kupitia programu ya Uanagenzi Pacha (Dual Apprenticeship training) katika chuo cha VETA Manyara. 
Washiriki wa warsha hiyo wakijadili jambo juu ya utekelezaji wa programu ya Uanagenzi Pacha (Dual Apprenticeship training)
Mkurugenzi wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi Bi. Stella Ndimubenya akichangia mada wakati wa warsha hiyo.
Baadhi ya washiriki wa warsha hiyo ambao ni wadau wa kilimo, ukarimu na utalii wakifuatilia mada wakati wa warsha hiyo. 

***************** 

Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imeendesha warsha kati yake na wadau wa sekta za Kilimo na Ukarimu na Utalii na kuweka mikakati ya kuzalisha wataalam mahiri wa sekta hizo kupitia programu ya Uanagenzi Pacha (Dual Apprenticeship Training System, DATS). 

Akifungua warsha ya wadau hao katika chuo cha VETA Manyara Desemba 30, 2020, Mkurugenzi Mkuu wa VETA Dkt. Pancras Bujulu amesema kuwa mafunzo kupitia programu hiyo yanamwezesha kijana kupata ujuzi wa fani husika akiwa chuoni na sehemu ya kazi, hivyo kumwezesha kwa kiasi kikubwa kujifunza kwa vitendo na kuendana na mahitaji ya soko la ajira pamoja na kupata uzoefu na uelewa wa mazingira halisi ya kufanyia kazi. 

Amesema wadau hao wana mchango mkubwa sana katika kuhakikisha mafunzo ya ufundi stadi yanatolewa kwa ufanisi na kuzalisha nguvukazi mahiri itakayochangia kuongeza tija na uzalishaji kwenye sekta hizo. 

VETA inatambua umuhimu wa kushirikiana na waajiri kwenye sekta mbalimbali kutoa mafunzo kwa kuwa ushirikiano huo unawezesha kuandaa nguvu kazi mahiri zaidi inayoendana na mahitaji halisi ya viwanda hasa kwa kuzingatia kuwa sehemu kubwa ya mafunzo hayo yanafanyika sehemu za kazi,amesema. 

Kwa mujibu wa Dkt Bujulu,programu hiyo imeendelea kufanya vizuri tangu kuanzishwa kwake mwaka 2012 kwa ushirikiano na Hamburg Chamber of Craft (HWK) ya Ujerumani ambapo jumla ya wanagenzi 448 wamefuzu mafunzo hayo kwenye fani za Ukarimu na Utalii, Ufundi Umeme, Ufundi Magari, Ujenzi, na Ufundi wa zana za kilimo. 

Dkt. Bujulu amewataka wadau hao kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa programu hiyo ili kuweza kuandaa wafanyakazi wenye viwango wanaohitajika katika kuleta mapinduzi katika sekta hizo. 

Mkurugenzi wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi Bi. Stella Ndimubenya amesema warsha hiyo imelenga kuwajengea uwezo wasimamizi wa mafunzo hayo viwandani, juu ya namna bora ya kutekeleza programu hiyo, kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto zitokanazo na utekelezaji wake. 

Mratibu wa programu hiyo Ndugu. Francis Komba amesema kuwa VETA imeamua kutoa mafunzo ya Uanagenzi pacha katika sekta hizo baada ya tafiti za soko la ajira kufanyika katika mikoa mbalimbali na kubaini mahitaji makubwa ya wataalamu wa hoteli na utalii pamoja na ufundi wa zana za kilimo kwa ngazi ya ufundi stadi. 

Balozi wa programu ya Uanagenzi pacha na Mkulima wa mjini Babati Ndugu Jitu Son ameishauri VETA kupanua wigo wa utoaji mafunzo ya ufundi stadi kupitia programu hiyo na kuwezesha vyuo vingi zaidi kutumia programu hiyo yenye manufaa makubwa kwa wanagenzi na waajiri. 

Mmoja wa wasimamizi wa programu hiyo ya Uanagenzi Pacha kutoka Moivaro Lodges, Serengeti Ndugu Musa Elphas amesema kuwa mfumo huo wa mafunzo umesaidia wenye hoteli kupata wafanyakazi bora zaidi kwa kuwa wenye hoteli wanapata fursa ya kushiriki kuwandaa wakati wa mafunzo. 

Naye msimamizi wa wanagenzi pacha kutoka TPC Ndugu Boniface Mwambaya amesema kuwa kiwanda chake kimefaidika na mafunzo hayo kwa kuwapata wanagenzi wanaofanya kazi kwa weledi na umakini. 

Mmoja wa wanufaika wa programu hiyo katika fani ya Ukarimuna Utalii Ndugu Azizi Ally amesema programu hiyo imemsaidia kupata ujuzi kwenye eneo la hoteli na kufanikiwa kujiajiri ambapo kwa sasa anamiliki Mgahawa wake na amefanikiwa kuajiri vijana wenzake wanne na hata sasa ameamua kupeleka vijana wawili kujiunga na mafuzo hayo kama mchango wake kwa jamii na kuwataka waajiri wenzake kuona umuhimu wa kuendelea kushiriki kutoa mafunzo hayo ya uwanagenzi pacha. 

Mfumo wa utoaji mafunzo ya Uanagenzi pacha unahusisha kuhudhuria mafunzo ya vitendo kwenye karakana na darasani (VETA) na kufanya vitendo zaidi katika sehemu za kazi. Mafunzo hayo ni ya miaka mitatu ambapo kwa kila mwaka mwanagenzi anatumia wiki 20 VETA na wiki 32 kwa mafunzo ya viwandani. 

Mfumo wa mafunzo ya Uanagenzi Pacha ulianzishwa mwaka 2011/12 kwa ushirikiano kati ya VETA na Hamburg Chamber of Crafts (HWK) ya Ujerumani, ambapo kwa sasa unatekelezwa katika vyuo vinne vya VETA vya Moshi RVTSC (Ukarimu na Utalii), Dar es Salaam RVTSC (Ufundi Umeme na Ufundi Magari), Simanjiro DVTC (Uashi) na Manyara RVTSC (Ufundi wa Zana za Kilimo). Viwanda na kampuni zaidi ya 150 zimenufaika na mafunzo hayo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments